Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 8 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 80 2016-11-09

Name

Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Primary Question

MHE. PROSPER J. MBENA aliuliza:-
Wananchi wa Wilaya ya Morogoro Vijijini kwa muda mrefu wamekuwa wakikosa huduma nzuri za matibabu katika hospitali ya Wilaya kama vile X-Ray, MRI, TSCAN dawa za kutosha, Madaktari Bingwa na Wauguzi kwa sababu tu Wilaya na Halmashauri yake zimechelewa kuhamia Mvuha suala ambalo Ofisi ya Rais, TAMISEMI inalishughulikia:-
(a) Je, Serikali itakuwa tayari kuanza kujenga Hospitali ya Wilaya Mvuha mahali ambapo ndipo patakapojengwa Makao Makuu ya Wilaya?
(b) Je, Serikali kwa sasa iko tayari kukiteua Kituo cha Afya cha Lukange ambacho ni bora sana kimejengwa na Kanisa Katoliki na kukikabidhi kitoe huduma kwa wananchi kama Hospitali Teule ya Wilaya ya Morogoro Kusini?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Prosper Joseph Mbena, Mbunge wa Morogoro Kusini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kusogeza huduma za afya karibu na wananchi, tayari Halmashauri imetenga eneo kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya katika eneo la Mvuha yatakapohamia Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro. Halmashauri inashauriwa kuweka katika vipaumbele vyake na kutenga bajeti katika mwaka wa fedha 2017/2018 ili kuanza ujenzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inakubaliana na wazo la kukifanya Kituo cha Afya Lukange kuwa Hospitali Teule ya Wilaya kwa kipindi cha mpito. Hata hivyo, suala hili linahitaji makubaliano baina ya Serikali na mmiliki wa kituo ambaye ni Kanisa Katoliki. Hivyo, tunashauri vikao vya maamuzi vya ngazi husika vya Mkoa na Wilaya, vikiona inafaa vianze mchakato huo mapema. Vikao hivyo, vikikaa na kuridhia pendekezo hilo, Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto haitasita kuteua kituo hicho kuwa Hospitali Teule ya Wilaya.