Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 9 Good Governance Ofisi ya Rais TAMISEMI. 98 2017-02-08

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Primary Question

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL aliuliza:-
Ushirika katika Wilaya ya Siha umekumbwa na matukio ya ufisadi yakiwemo upotevu wa zaidi ya shilingi milioni 840 katika Ushirika wa Siha Kiyeyu, upotevu wa shilingi milioni 337 ya SACCOS ya Sanya Juu pamoja na matumizi mabaya ya ardhi, licha ya uchunguzi mzuri uliofanywa na TAKUKURU Mkoa:-
Je, ni kwa nini uchunguzi huo unaingiliwa na maslahi binafsi ya watu wachache na kusababisha matukio yanayodhalilisha Serikali?

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UTUMISHI NA UTAWALA BORA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii kujibu swali lililoulizwa na Mheshimiwa Dkt. Godwin Oloyce Mollel, Mbunge wa Jimbo la Siha, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kifungu cha 5 (2) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ya Mwaka 2007, TAKURURU imepewa mamlaka kuwa chombo huru cha kuzuia na kupambana na rushwa nchini; na inatekeleza majukumu yake muhimu kama yalivyofafanuliwa katika Kifungu cha (7) cha sheria hiyo ya kuzuia na kupambana na rushwa. Kutokana na mantiki hiyo ya kisheria, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa namna yoyote ile, Taasisi ya TAKUKURU haiwezi kuingiliwa na mtu yeyote.
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba TAKUKURU ilipokea tuhuma za udanganyifu wa matumizi ya fedha za umma kutoka katika vyanzo vyake mbalimbali zilizokihusu Chama cha Ushirika cha Siha Kiyeyu na Sanya Juu SACCOS. Kutokana na tuhuma hizo, uchunguzi uliofanywa na TAKUKURU ulithibitisha pasipo shaka kwamba viongozi wa Chama cha Ushirika Siha Kiyeyu bila ridhaa ya wanachama wake, waligawa mashamba kwa watu wasio wanachama wapatao 13, shamba lenye ekari 16 ambazo zililimwa kati ya miaka miwili na mitano bila ya kulipiwa gharama yoyote. Kitendo hiki kiliukosesha ushirika Siha Kiyeyu mapato ya kiasi cha sh. 1,600,000/=.
Mheshimiwa Spika, uchunguzi pia ulithibitisha pasipo shaka kwamba uongozi wa Chama cha Msingi cha Ushirika cha Siha Kiyeyu ulitoa maelezo ya uongo kwa Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mheshimiwa William Olenasha kwa kumpatia stakabadhi za uongo juu ya matumizi ya sh.500,000/= za ushirika kwa ajili ya semina. Baada ya uchunguzi kukamilika uongozi huo ulikiri kutenda kosa hilo mbele ya wachunguzi.
Mheshimiwa Spika, tuhuma kuhusu ufisadi wa sh.337,000/= unaoihusu SACCOS ya Sanya Juu ni tuhuma mpya. Tuhuma za Sanya Juu SACCOS zilihusu kiasi cha sh.160,100,406, na tuhuma hizi zilichunguzwa na Jeshi la Polisi na kesi Na. CC 15/2016 imeshafunguliwa na ipo katika Mahakama ya Wilaya ya Siha.
Mheshimiwa Spika, tuhuma za upotevu wa shilingi milioni 840 unaokihusu Chama cha Ushirika cha Kiyeyu ni malalamiko ya wanachama juu ya tozo anazolipa mwekezaji katika shamba la maparachichi ambapo anadaiwa kulipa kiasi cha shilingi milioni 60 kwa mwaka. Tuhuma hizi ni mpya na Ofisi ya TAKUKURU Mkoa wa Kilimanjaro imezipokea kwa ajili ya uchunguzi zaidi. Uchunguzi utakapokamilika, taarifa itatolewa.