Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 10 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 110 2017-02-10

Name

Haji Khatib Kai

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Micheweni

Primary Question

MHE. ALLY SALEH ALLY (k.n.y. MHE. HAJI KHATIB KAI) aliuliza:- Arusha International Conference Center ni miongoni mwa taasisi ya iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki baada ya kuvunjika kwa Jumuiya hiyo mwaka 1977, hivyo hii inaonyesha kwamba taasisi hiyo ina sura ya Muungano. Je, ni kwa nini taasisi hii haionyeshi ushiriki wa Zanzibar?

Name

Dr. Susan Alphonce Kolimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:- Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ruhusa yako na kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Haji Khatib Kai, Mbunge wa Micheweni kama ifuatavyo:- Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC), kilianza shughuli zake rasmi tarehe 1 Julai, 1978 kufuatia kuvunjika kwa Jumuiya ya awali ya Afrika Mashariki mwaka 1977. Kituo hicho kilianzishwa kwa kuzingatia Sheria mama ya Mashirika ya Umma ya mwaka 1969 kwa kupitia establishment order iliyotolewa kupitia notice ya Serikali Na. 115 ya tarehe 25 Agosti, 1978. Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo hicho pamoja na Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere vimemilikishwa kupitia Notisi ya Serikali Na. 84 ya tarehe 4 Aprili, 2014, ambapo vituo vyote vipo chini ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Kituo kilianza shughuli zake kikiwa na madhumuni makubwa mawili ambayo ni kuendesha biashara ya mikutano na upangishaji wa nyumba na ofisi. Mheshimiwa Mwenyekiti, kimuundo Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi huteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo Wajumbe wa Bodi huteuliwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Kwa kutambua umuhimu wa ushiriki wa Zanzibar katika uendeshaji wa kituo kama taasisi ya Muungano, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki huwa wakati wote anamteua Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi kutoka Zanzibar ili kuhakikisha ushiriki wao katika kituo hicho. Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo kinafanya kazi chini ya Bodi ya Wakurugenzi na shughuli za uendeshaji za kila siku zinasimamiwa na Mkurugenzi Mwendeshaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile pale inapotokea fursa ya ajira katika nafasi za utendaji, nafasi hutolewa kwa ushindani na hutangazwa kupitia magazetini ambapo pande zote mbili za muungano huchangamkia nafasi hizo na washindi hupatikana kulingana na uwezo wao katika nafasi walizoomba.