Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 2 Energy and Minerals Wizara ya Madini 14 2017-04-05

Name

Capt. (Mst). George Huruma Mkuchika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjini

Primary Question

MHE. KAPT. (MST.) GEORGE H. MKUCHIKA Aliuliza:-
Serikali iliwaahidi wananchi wa Mikoa ya Mtwara na Lindi umeme wa uhakika na wa kutosha baada ya kugundulika kwa gesi na baada ya neema ya muda mfupi hivi sasa kuna tatizo kubwa la kukatika kwa umeme mara kwa mara katika Mikoa hiyo ikiwemo na Wilaya ya Newala.
Je, tatizo ni nini na Serikali inachukua hatua gani kumaliza kabisa tatizo hili?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kepteni Mstaafu George Huruma Mkuchika, Mbunge wa Newala Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya kukatika kwa umeme mara kwa mara katika maeneo ya Mikoa ya Lindi na Mtwara inatokana na ubovu wa jenereta moja kati ya tisa katika kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia kilichoko Mtwara chenye jumla ya MW 18 ambayo imepungua hadi MW 16. Tatizo lingine ni uchakavu na urefu wa njia inayosambaza umeme wa msongo wa kilovoti 33 kutoka Mtwara kuelekea Wilaya za Mtwara – Tandahimba – Newala – Masasi – Nanyumbu- Nachingwea hadi Ruangwa ambao ni umbali wa kilometa 206.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua zinazochukuliwa na Serikali ili kuondoa tatizo hilo ni pamoja na kufanya ukarabati wa mtambo ulioharibika ili kurudisha uwezo wa kituo katika kuzalisha hali yake ya kawaida MW 18. Kazi hii inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Mei, 2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango mwingine ni kuongeza mitambo mingine sita yenye uwezo wa kuzalisha umeme wa jumla ya MW 12 kila moja itakayofikisha MW 30 ambao unatosheleza kwa mahitaji ya mikoa hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha hali ya upatikanaji endelevu wa umeme katika Mikoa hiyo, TANESCO inajenga njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 132 yenye urefu wa kilometa 80 kutoka Mtwara hadi Mnazi Mmoja, Lindi. Kazi hiyo inajumuisha pia ujenzi wa vituo vya kupoza umeme msongo wa kilovoti 132/33 na transfoma za MVA 20 kwa ajili ya kusambaza umeme wa njia tano. Mradi huu unakamilika mwishoni mwa mwezi Mei, mwaka huu na gharama za mradi huu ni shilingi bilioni 16.