Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 2 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 18 2017-04-05

Name

Joseph Kasheku Musukuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita

Primary Question

MHE. MUSUKUMA J. KASHEKU Aliuliza:-
Wakala wa Misitu Tanzania amehamisha vigingi vya mipaka ya misitu vilivyowekwa tangu mwaka 1974 na kuviweka katikati ya vijiji kwa kufuata ramani ya mwaka 1984, vijiji ambavyo vina GN ya Serikali na vinatambuliwa na hata Mheshimiwa Rais amezuia zoezi hilo, lakini hakuna
kilichofanyika hivyo kuwafanya wananchi wa vijiji hivyo kuishi maisha ya mashaka na sintofahamu.
Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya tatizo hilo?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Musukuma Joseph Kasheku, Mbunge wa Geita, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Msitu wa Hifadhi wa Geita wenye ukubwa wa hekta 47,700 ulisajiliwa kwa ramani namba Jb 146 ya mwaka 1952 na ulitangazwa rasmi kwa Tangazo la Serikali Namba 110. Sehemu kubwa ya msitu huu ipo kwenye miteremko ya milima ya Geita inayozunguka mji wa Geita sehemu ya Magharibi, Kaskazini na Kaskazini Mashariki.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1984 Serikali ilifanya mapitio ya soroveya ya mipaka ya msitu kwa lengo la kuweka alama kwa kutumia ramani iliyoanzisha msitu huo. Katika mapitio hayo ilibainika kuwa mpaka halisi wa msitu kwa mujibu wa sheria umepita katikati ya vijiji vilivyoanzishwa na kusajiliwa mwaka 1974 wakati wa operation vijiji. Alama za mipaka zikawekwa kufuata mpaka huu halisi na hivyo kusababisha eneo ambalo wananchi walikuwa wameanza kuishi na kufanya shughuli za kibinadamu na baadaye kusajiliwa kuwa vijiji kuangukia ndani ya eneo la msitu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kubaini tatizo hilo Serikali haijafanya operation yoyote ya kuwaondoa wananchi katika maeneo hayo, bali ipo katika mjadala unaotafuta njia za kutatua tatizo hili bila ya kuleta athari hasi na kubwa kwa maisha ya wananchi. Aidha, Mheshimiwa Mbunge anashauriwa kuwa na subira wakati Wizara yangu kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Geita inaendelea kutafuta suluhisho la mkanganyiko uliojitokeza kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo.