Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 12 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 104 2017-04-25

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Primary Question

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza:-
Kati ya mwaka 1954 na 1957 kulifanyika zoezi la upimaji wa maeneo ya Hifadhi za Misitu, Mapori ya Akiba na Hifadhi katika Wilaya ya Sikonge ambapo kulikuwa na wakazi takribani 16,000 na ng’ombe wapatao 2500. Kwa sasa wakazi wameongezeka hadi kufikia takribani 300,000 na ng’ombe wapo takribani 200,000 lakini eneo la kuishi, kulima na malisho ya mifugo na shughuli nyingine za kiuchumi ni lile lile la asilimia 3.7 ya eneo lote la Wilaya huku eneo la Hifadhi likibaki asilimia 96.3 na hali hii inasababisha migogoro kati ya wakulima, wafugaji na warina asali dhidi ya Maafisa Maliasili.
(a) Je, ni lini Serikali itawaongezea wakazi wa Wilaya ya Sikonge eneo la kuisha, kulima na kulishia mifugo kutoka asilimia 3.7 hadi angalau asilimia 25 ya eneo lote la Wilaya?
(b) Je, Serikali haioni kuwa kuongeza eneo la Wilaya hiyo kwa asilimia 25 kutaepusha migogoro iliyopo sasa na hivyo wananchi watatekeleza shughuli zao kwa amani na utulivu huku wakilinda mazingira pamoja na hifadhi?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, lenye sehemu (a) na
(b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na takwimu za Taasisi ya Takwimu ya Taifa (The National Bureau of Statistics) na Sensa ya mwaka 2012, Wilaya ya Sikonge ina ukubwa wa kilometa za mraba 27,873 na idadi ya watu wapatao 179,883. Aidha, maeneo ya hifadhi za misitu na wanyamapori yana ukubwa kilometa za mraba 20,056.94 sawa na asilimia 72 ya eneo lote la Wilaya, hivyo kufanya eneo la makazi na shughuli nyingine za binadamu kuwa sawa na asilimia 28.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hifadhi za misitu na mapori ya akiba katika Wilaya ya Sikonge ni muhimu kwa uhifadhi na maendeleo ya sekta nyingine, ikiwa ni pamoja na kuwa vyanzo vya mto Ugalla, ziwa Sagara, Nyamagoma na ardhi oevu ya Malagarasi - Moyowosi. Kwa mantiki hiyo, kugawa maeneo haya na kuruhusu shughuli za kibinadamu kutahatarisha upatikanaji wa rasilimali za maji kwa ajili ya shughuli za uvuvi, kilimo, ufugaji, matumizi ya nyumbani na mengineyo kwa kiasi kikubwa. Muhimu zaidi ni mchango mkubwa wa misitu hiyo katika hali ya hewa na udhibiti wa mabadiliko hasi ya tabianchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imethibitika kwamba kilimo cha kuhama hama, ikiwa ni pamoja na utumiaji wa maeneo makubwa ya ardhi; ufugaji wa kuhama hama ukijumuisha uingizaji wa mifugo katika maeneo yaliyohifadhiwa, ni matumizi mabaya ya rasilimali ardhi na yasiyo na tija kwa Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi nitumie nafasi hii kuwakumbusha na kuwaomba wananchi kwa kushirikiana na uongozi wa Halmashauri za Wilaya husika, kuchukua hatua za makusudi kuandaa na kutekeleza mipango ya matumizi bora ya ardhi; hatua ambazo zitasaidia kuondoa changamoto za mahitaji ya ardhi katika Wilaya zote nchini ikiwa ni pamoja na Wilaya ya Sikonge iliyoko Mkoani Tabora.