Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 25 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 200 2017-05-15

Name

Leonidas Tutubert Gama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Primary Question

MHE. LEONIDAS T. GAMA aliuliza:-
Wananchi wa Songea Mjini wamekuwa wakiitumia Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma kama Hospitali yao ya Wilaya hivyo kufanya kuwepo na mgongano wa kiutendaji kati ya Mamlaka ya Mkoa inayoitambua Hospitali hiyo kama Rufaa ya ngazi ya Mkoa na Mamlaka ya Wilaya. Tarehe 10 Januari, 2016, Mheshimiwa Waziri wa Afya alifika kuona hali halisi na juhudi za wananchi wa Songea Mjini za kujenga Kituo cha Afya Mji Mwema ambacho kimefikia hatua kubwa, hivyo wakamwomba Waziri kituo hicho kipandishwe hadhi kuwa Hospitali ya Wilaya, Songea Mjini.
(a) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuiacha Hospitali ya Mkoa ifanye kazi ya Rufaa Kimkoa?
(b) Je, Serikali haioni haja ya kupunguza msongamano katika hospitali hiyo kwa kuanzisha Hospitali ya Wilaya Songea Mjini?
(c) Je, ni lini basi Serikali itakipa hadhi Kituo cha Afya cha Mji Mwema, Songea Mjini ya kuwa Hospitali ya Wilaya?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: alijibu: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leonidas Tutubert Gama, Mbunge wa Songea Mjini, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma inatakiwa kutoa huduma za rufaa kama inavyofanyika kwa Hospitali zote za Mikoa nchini. Hata hivyo, mahali ambapo hakuna Hospitali ya Wilaya, wagonjwa hawazuiliwi kwenda katika Hospitali ya Mkoa kwa ajili ya matibabu. Mpango uliopo ni kuimarisha Zahanati na Vituo vya Afya ndani ya Halmashauri ili viweze kutoa huduma kwa wagonjwa wengi ili kupunguza msongamano katika Hospitali hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inakusudia kuboresha Kituo cha Afya cha Mji Mwema ili kiweze kutoa huduma bora za matibabu kwa lengo la kupunguza msongamano katika Hospitali ya Mkoa kwa sasa. Serikali itatoa kipaumbele kwa mpango wowote wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea juu ya uanzishwaji wa Hospitali ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya cha Mji Mwema kimeshaombewa kibali kuwa Hospitali. Timu ya Wataalam kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeshakagua kituo na kuelekeza yafanyike maboresho ya miundombinu inayohitajika ili kiweze kukidhi vigezo vya kuwa hospitali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Fedha na Mipango ya Halmashauri ya Manispaa ya Songea, imepanga kukutana tarehe 17 Mei, 2017 ili kujadili utekelezaji wa maelekezo ya Wizara ya Afya.