Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 4 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 34 2016-04-22

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

Halmashauri ya Mbeya ina vijiji vingi ambavyo havijapata umeme katika Mpango wa REA na pia utekelezaji wa REA II uko nyuma sana:-
(a) Je, ni vijiji vingapi vya Halmashauri ya Mbeya vimo kwenye REA II na mradi utakamilika lini?
(b) Je, Kwa nini mradi wa REA II haujalenga kupeleka umeme kwenye huduma za kijamii kama vile Shule, Zahanati, Nyumba za ibada na vyuo?
(c) Je, ni lini sasa vijiji vilivyobaki vitapewa umeme wa REA?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vya Halmashauri ya Mbeya vilivyomo kwenye REA Awamu ya Pili ni 27, vikiwemo vijiji vya Chang’ombe, Hatwelo, Haporoto, Idimi, Kasele, pamoja kijiji cha Wambishe.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi unaotekelezwa katika Awamu ya Pili , unafanywa na Mkandarasi SINOTEC ambao umefikia asilimia 54.33 na mradi huu unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2016/2017.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika miradi yote inayotekelezwa na Serikali kupitia Mfuko wa REA Vijijini, kipaumbele kimewekwa kwenye huduma za kijamii kama vile shule, zahanati, vituo vya afya, nyumba za ibada na mashine za kusukuma maji. Katika Mpango wa Awamu ya Pili ya umeme vijijini maeneo ya huduma za jamii ambayo yatafikishwa huduma ya umeme katika Halmashauri ya Mbeya Vijijini ni pamoja na shule za msingi 23, shule za sekondari tano, zahanati 10, kituo cha afya kimoja, pamoja na nyumba za ibada 42.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vingine vya Mbeya Vijijini ambavyo havikupata umeme kwenye Mpango wa REA kabambe Awamu ya Pili, vimewekwa kwenye Awamu ya Tatu unayotarajiwa kutekelezwa mara baada ya bajeti hii ya mwaka 2016 kupitishwa na Waheshimiwa Wabunge. Jumla ya vijiji 111 katika kata 30 za Mbeya Vijijini vimejumuishwa katika REA Awamu ya Tatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme kwenye maeneo yanayojumuisha ujenzi wa shule za umeme pamoja na zahanati, inafanyika kwa ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 480; ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 530, ufungaji wa transfoma 137 za ukubwa mbalimbali pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 7,465. Gharama ya kazi hii inakadiriwa kufikia shilingi bilioni 51.52