Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 37 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 301 2017-05-30

Name

Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Primary Question

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza:-
Kati ya mwezi Juni – Desemba, 2015 wananchi wapatao sita walishambuliwa na kuuawa na wanyamapori na Shirika la Hifadhi Tanzania (TANAPA) halikushiriki mazishi ya watu hawa, wala hakuna fidia yoyote waliyopata ndugu wa marehemu, hali inayoonesha mahusiano mabaya kati ya jamii na Mamlaka ya Hifadhi, zaidi ya hayo wanyama kama tembo, wamesababisha hasara kubwa sana kwa kuharibu mazao katika Tarafa ya Daudi, Kata za Marangwa, Daudi, Bargish na Gehandu.
• Je, ni lini Serikali itawalipa fidia ndugu wa hao watu sita waliouawa na wanyama wakali katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu?
• Je, ni lini Serikali kupitia TANAPA italipa fidia kwa wale wote walioharibiwa mazao shambani mwaka 2014/ 2015?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaya, Mbunge wa Mbulu Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hailipi fidia kwa madhara yanayosababishwa na wanyamapori hatari au waharibifu, badala yake inatoa kifuta jasho au kifuta machozi, kwa mujibu wa kifungu cha 68(1) cha Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009. Aidha, kifungu cha (3) cha Kanuni za Malipo ya Kifuta Jasho na Kifuta Machozi za mwaka 2001 kinaainisha masharti na viwango vya malipo ya kifuta jasho na kifuta machozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu imepokea madai ya wananchi watano waliouawa, wanne walijeruhiwa na 31 walioharibiwa mazao yao katika eneo ambalo Mheshimiwa Mbunge analizungumzia. Madai hayo yamefanyiwa kazi kwa mujibu wa kanuni na yatalipwa mara fedha zitakapopatikana.