Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 1 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 04 2017-11-07

Name

Hassan Elias Masala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Primary Question

MHE. HASSAN E. MASALA aliuliza:-
• Je, Serikali kupitia REA III ina mpango gani wa kusambaza umeme katika kata zilizobaki Wilayani Nachingwea?
• Je, nini mpango wa Serikali kutatua tatizo la kukatikakatika kwa umeme Wilayani Nachingwea?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu, nimshukuru pia Mheshimiwa Rais kwa imani yake na nikushukuru wewe pia Mheshimiwa Spika kwa uongozi wako.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Elias Masala, Mbunge wa Nachingwea, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kuwa vijiji vyote visivyo na umeme vinapata umeme kupitia mradi kabambe wa kupeleka umeme vijijini Awamu ya Tatu (REA III) unaotegemewa kukamilika mwaka 2020/2021. Mradi huu utajumuisha vipengele vitatu vya Densification, Grid Extension na Off-Grid Renewables. Mkoa wa Lindi chini ya Mradi wa Uendelezaji wa Gridi mzunguko wa Kwanza unatekelezwa kwa muda wa miezi 24 na Kampuni ya State Grid & Technical Works Ltd. Katika Wilaya ya Nachingwea Mpango wa Awamu ya Tatu utavipatia umeme vijiji 30. Kazi za utekelezaji wa mradi zilianza mwezi Julai, 2017 na zitakamilika Juni 30, 2019. Aidha, vijiji vilivyobakia vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa REA III utakaoanza Aprili, 2019 hadi Disemba 2021.
Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme mzunguko wa kwanza itajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 380, ufungaji wa transfoma 180, ujenzi wa njia za msongo wa kilovoti 0.4 zenye urefu wa kilometa 360 na uunganishaji wa wateja wapatao 5,710 katika Mkoa mzima wa Lindi. Aidha, kwa Wilaya ya Nachingwea jumla ya wateja wapatao 1,200 wataunganishwa. Mkandarasi anaendelea na upimaji wa njia za umeme ambapo amefikia asilimia 30 na kazi za upimaji zitakamilika mwishoni mwa Novemba, 2017. Gharama za miradi hiyo ni jumla ya shilingi 24,636,112,764.82 na dola za Kimarekani 5,657,471.30 pamoja na VAT.
(b) Mheshimiwa Spika, umeme unaotumika katika Wilaya ya Nachingwe unatoka katika kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia kilichopo Mtwara Mjini ambapo njia ya kusafirisha umeme kutoka Mtwara ina urefu wa kilometa 210 na pia hugawa umeme katika maeneo ya Mkoa wa Mtwara kabla ya kufika Nchingwea. Hivyo, pakitokea tatizo lolote mwanzoni au katikati ya njia basi, umeme hukatika katika maeneo mengi ya Mkoa wa Lindi, ikiwemo Nachingwea. Ili kukabiliana na tatizo hilo Serikali kupitia TANESCO imejenga njia mpya ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 132 kutoka Mtwara hadi Mnazi Mmoja, Lindi na kujenga kituo cha kupoza umeme chenye uwezo wa MVA 20, 132/33kV ambapo ujenzi wake umekamilika na mradi mzima umegharimu jumla ya shilingi bilioni 16.
Mheshimiwa Spika, umeme utapozwa katika msongo wa kilovoti 33 na kusafirishwa kwenda katika Wilaya za Ruangwa, Nachingwea na badae Liwale. Ujenzi wa njia ya msongo wa kilovoti 33 ya Wilaya ya Ruangwa unategemewa kuanza Januari, 2018 baada ya kupatikana kwa fedha za utekelezaji. Pamoja na ujenzi huo, ukarabati wa miundombinu iliyopo unaendelea ili kuboresha mfumo mzima wa usambazaji katika Wilaya ya nachingwea na Lindi kwa ujumla.