Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 1 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 13 2017-11-07

Name

Deogratias Francis Ngalawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Primary Question

MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA aliuliza:-
Wafanyakazi wa TTCL wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki waliolipwa pesheni ni wale waliofungua kesi mahakamani na kushinda. Aidha, wapo ambao wanastahili malipo lakini hawakuwa na uwezo wa kumlipa Wakili katika kuendesha kesi hiyo.
Je, ni lini Serikali itawalipa wafanyakazi wa TTCL wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki madai ya pesheni zao?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Wiziri ya Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deogratias Francis Ngalawa, Mbunge wa Ludewa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, siyo kweli kwamba wafanyakazi wa TTCL wa iliyokuwa Jumuiya ya Mashariki waliolipwa pesheni ni wale tu waliofungua kesi mahakamani. Kumbukumbu zinaonyesha kwamba tarehe 31 Disemba, 1990 Serikali ilisitisha mfuko wa ujulikanao kama East Africa Non Countributory Pension Scheme baada ya kushauriana na kukubaliana na Menejimenti pamoja na Chama cha Wafanyakazi wa TTCL wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Baada ya kusitishwa kwa mfuko huo kila mfanyakazi alilipwa asilimia 50 ya michango yake na asilimia 50 iliyobaki ilipelekwa NSSF kwa ajili ya pesheni ya kila mwezi pindi watakapostaafu. Ni vema ikafahamika kwamba, wafanyakazi wote wa TTCL wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki wanalipwa pesheni zao na NSSF baada ya kustaafu.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, baada ya malipo ya asilimia 50 kwa 50 kukamilika, wafanyakazi 254 hawakuridhika na maamuzi ya Serikali ya kusitisha mfuko wa East African Non Countributory Pension Scheme na kufungua kesi Na. 69/ 2005 Mahakama Kuu kupinga maamuzi ya Serikali. Katika shauri hilo, Mahakama Kuu iliamua kuwa uamuzi wa Serikali kusitisha mfuko huo haukuwa sahihi kisheria na hivyo wafanyakazi 254 waliokuwa katika shauri hilo walipwe madai yao ambayo yalijumuisha malipo ya mkupuo, riba pamoja na pensheni ya kila mwezi ya wafanyakazi hao.
Mheshimiwa Spika, baada ya uamuzi huo wa Mahakama Kuu, Hati ya Makubaliano (Deed of Settlement) yenye tuzo ya shilingi 13,685,450,397.82 ilisainiwa mnamo tarehe 27 Agosti, 2013 na kusajiliwa Mahakama Kuu ya Tanzania, Dar es Salaam mnamo tarehe 2 Agosti, 2013 ikiwa ni tuzo kwa wafanyakazi wote waliofungua shauri husika. Aidha, mahakama ilielekeza kuwa wadai katika kesi hiyo ambao bado wako kazini malipo yao yatafanyika mara baada ya kustaafu. Kwa mujibu wa Hati ya Makubaliano malipo yaligawanywa katika awamu tatu ambapo hadi kufikia Julai 2017 awamu zote tatu zimelipwa jumla ya shilingi 12,665,994,447.92.
Mheshimiwa Spika, hadi sasa wastaafu 245 wameshalipwa madai yao yote ya fedha za mkupuo ambapo kati yao wastaafu 54 wamefariki dunia na fedha zao walilipwa warithi na wastaafu 198 wanaendelea kulipwa malipo ya nyongeza ya pensheni ya kila mwezi. Kwa upande wa wadai ambao bado wapo kazini amebaki mmoja na wengine wawili wamestaafu hivi karibuni na tunatarajia kuwaombea fedha zao mwezi huu wa Novemba, 2017.
Mheshimiwa Spika, baada ya Mahakama Kuu kutoa uamuzi huo, lilijitokeza kundi lingine la wastaafu wa TTCL waliokuwa chini ya Jumuiya ya Afrika Mashariki likiongozwa na Bwana L. Mwayela na wenzake 324 na kuomba kuunganishwa katika Deed of Settlement ya kesi Na 69/2005 kati ya Bwana Berekia G. Mkwama na wenzake 254 dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kwa kuwa Mahakama Kuu iliamua pamoja na mambo mengine kuwa wafanyakazi waliofungua kesi hiyo ndiyo walipwe madai yao na kwamba Deed of Settlement iliyosajiliwa Mahakamani ilihusisha wafanyakazi waliofungua kesi hiyo tu, wafanyakazi wengine ambao hawakuwa sehemu ya kesi hiyo hawawezi kulipwa kwa kutumia hukumu na tuzo ya kesi ambayo hawakuwa sehemu yake. Kwa msingi huo, Serikali haiwezi kulipa madai mengine ambayo hayajathibitika kisheria.