Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 17 2017-11-08

Name

Anna Richard Lupembe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza:-
Kijiji cha Mtisi katika Kata ya Sitalike hakuna eneo la kilimo:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapa wananchi hao maeneo kwa ajili ya kilimo?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Mtisi kilichopo katika Kata Sitalike, Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kina eneo la ardhi lenye jumla ya hekta 1,066.86. Kati ya hizo, hekta 1,043.86 ni sehemu ya Hifadhi ya Msitu wa Msaginya unaomilikiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS). Maana yake ni kwamba, jumla ya kaya 589 zenye wakazi 3,416 wa kijiji hicho wamebakia na eneo la hekta 23 tu wanaloruhusiwa kulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mahitaji ya ardhi ya kilimo katika kijiji hicho ni hekta 919.4, Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo, ifikapo mwishoni mwa Novemba, 2017, itakuwa imewapatia ardhi wakazi hao kutoka katika Kijiji cha Stalike (Makao Makuu ya Kata ya Sitalike) chenye ardhi ya ziada hekta 2,950.