Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 5 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 59 2017-11-13

Name

Shamsia Aziz Mtamba

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Mtwara Vijijini

Primary Question

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA aliuliza:-
Katika Mkoa wa Mtwara kuna tatizo kubwa la kukatika kwa umeme mara kwa mara jambo ambalo linaathiri wananchi ikiwemo wafanyabiashara ambao wanategemea sana umeme na hivyo kusababisha wakati mwingine biashara hizo kuharibika na kuwasababishia hasara wananchi hao.
Je, ni lini Serikali itawahakikishia wananchi wa Mtwara kupata umeme wa uhakika?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Shamsia Aziz Mtamba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini wanapata umeme wa uhakika ili kuboresha maisha yao. Serikali kupitia TANESCO imeweka jitihada kubwa kuhakikisha kuwa umeme wa kutosha katika Mikoa ya Mtwara na Lindi unapatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kufanya ukarabati mkubwa wa mitambo yote tisa iliyopo Mtwara yenye uwezo wa kuzalisha megawati 18. Ukarabati huu ulianza mwishoni mwa mwezo Oktoba, 2017 na utakamilika mapema mwezi Desemba, 2017. Gharama ya matengenezo kwa mitambo yote ni shilingi 4,800,000,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ukarabati huo, Serikali imeagiza mitambo miwili mipya kutoka Kampuni ya Caterpillar yenye uwezo wa kuzalisha jumla ya megawati nne kwa gharama ya shilingi 8,300,000,000. Ufungaji wa mitambo hiyo unatarajiwa kuanza mwezi Januari, 2018 na kukamilika mwezi Aprili, 2018. Mitambo hiyo itaongeza uwezo wa mashine zilizopo kufikia megawati 21.75.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO imeanza utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa megawati 300 kwa kutumia gesi asilia Mkoani Mtwara. Kazi inayoendelea kwa sasa ni kukamilisha upembuzi yakinifu kupitia Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Japani (JICA). Mradi huo unategemewa kuanza mwezi Aprili, 2018 na kukamilika mwezi Desemba, 2019. Mradi huu utakapokamilika utatoa suluhisho la kudumu la upatikanaji wa umeme wa kutosha katika Mikoa ya kusini ikiwa ni pamoja na Lindi na Mtwara.