Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 6 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 81 2017-11-14

Name

Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Primary Question

MHE. JOSEPH L. HAULE aliuliza:-
Wanyama hasa Tembo wamekuwa wakiharibu sana mazao ya wananchi kwa fidia ndogo sana ya Sh. 20,000 kwa heka na hii hupunguza ushiriki wa wananchi katika kuzuia ujangili ndani ya Hifadhi:-
Je, Serikali imejipangaje kukaa vizuri na wananchi wa vijiji vinavyopakana na Hifadhi ili kuwa na ushirikiano katika kuzuia ujangili?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Leonard Haule, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa maisha ya binadamu, mazao na mifugo imeweka utaratibu wa kulipa kifuta jasho na machozi kwa uharibifu unaosababishwa na wanyamapori wakali na waharibifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali kupitia halmashauri zake za Wilaya na taasisi zilizo chini ya Wizara ya maliasili na utalii imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kuelimisha jamii kuhusu uhifadhi na sheria zake ikwemo za kufukuza wanyamapori mara inapotokea wameingia katika makazi ya wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara itaendelea kushirikiana na wadau wa uhifadhi kutoa elimu kwa wananchi juu ya kutumia pilipili na ufugaji wa nyuki kandokando ya mashamba ili kuzuia wanyama hususani tembo kuingia mashambani. Elimu hii ilianza kutolewa katika vijiji vinavyopakana na Hifadhi ya Taifa ya Mikumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ili kufanya zoezi hili kuwa endelevu vikundi 23 vilisaidiwa kuanzisha Mfuko wa Kuweka na Kukopa na fedha wanayopata isaidie kununua baadhi ya vifaa vinavyotumika kuzuia wanyama kuingia mashambani pamoja na kuviwezesha vikundi kiuchumi ili visaidiwe katika kuzuia ujangili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya vikundi vilivyoanzishwa, kumi vimepata usajili toka halmashauri ya wilaya na vingine 13 bado vinaendelea kushughulikia usajili wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imetoa mizinga 180 kwa wananchi wa Kijiji cha Maharaka ikiwa ni kuunga mkono juhudi zinazofanywa na wananchi katika kutekeleza maazimio ya kutumia pilipili na mizinga ya nyuki kuzuia tembo kuingia katika mashamba yao. Vilevile elimu inaendelea kutolewa katika Vijiji vya Mikumi, Mkata na Ihombwe ili nao kutumia mfumo wa pilipili katika mashamba yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuzishauri Halmashauri za Wilaya kuajiri Askari Wanyamapori na kuwapatia vitendea kazi ili waweze kusaidia wananchi pale kunapojitokeza tatizo la uharibifu wa mazao na mifugo kuvamiwa na wanyamapori.