Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 10 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 19 2018-01-31

Name

Desderius John Mipata

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkasi Kusini

Primary Question

MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-
Wananchi wa Kata ya Nkandasi wamejitahidi kujenga shule ya Sekondari ya Kata ya Milundikwa hadi kufikia kidato cha sita lakini Serikali kupitia Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa imeamuru shule hiyo kuhamishwa mara moja kuanzia tarehe 1 Januari, 2017 kuachia Jeshi:-
(a) Wananchi walitumia muda na rasilimali zao kukamilisha ujenzi huo na sasa wanakwenda kuanza upya: je, ni upi mchango wa Wizara kwa ujenzi mpya wa shule?
(b) Wizara ya Elimu imeafiki kuhamishwa shule hiyo ya Kata; Je, ni upi mchango wa Wizara katika uhamishaji wa shule hiyo?
(c) Je, Serikali iko tayari kufanya uthamini wa miundombinu yote ya shule na majengo, yaliyojengwa na wananchi na thamani hiyo kuitoa katika fedha taslimu kwa ujenzo wa shule mpya?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deusderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na Jeshi la Kujenga Taifa kuhitaji eneo lao ilipokuwa imejengwa shule ya sekondari ya Milundikwa kuanzia Januari 2017, Serikali ilihamishia shule hiyo kwenye eneo jipya la Kijiji cha Kasu A. Ushirikiano mzuri baina ya Serikali Kuu, Halmashauri, JKT, Mbunge na wananchi umewezesha ujenzi wa madarasa 13, vyoo matundu 26 na bweni moja kukamilika. Ujenzi wa maabara moja ya sayansi na bweni la pili uko katika hatua za mwisho ambapo wanafunzi 461 wakiwepo 92 wa kidato cha tano wanasoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kuchangia shilingi milioni mbili na wananchi wa Kata ya Nkandasi hususan Vijiji vya Katani, Kisula, Malongwe, Milundikwa, Kasu A na Kasu B kwa kujitolea kuchimba msingi, kukusanya mawe na mchanga, kuteka maji kwa ajili ya ujenzi kwa utaratibu wa 50 kwa 50 yaani wanaume 50, wanawake 50 kila siku ya ujenzi na kufyatua tofali za kuchoma laki mbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi nayo ilitoa milioni arobaini na tisa kwa ajili ya ujenzi huo na Serikali Kuu kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ilitoa shilingi milioni mia mbili hamsini na tisa zilizotumika kujenga vyumba vya madarasa manne, vyoo matundu 22 na mabweni mawili ambapo ujenzi wa bweni la pili unaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia ukamilishaji wa bweni la pili, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa mwezi Desemba, 2017 imepeleka shilingi milioni mia moja na Jeshi la Kujenga Taifa nalo lilichangia mabati 204, miche 300 ya miti kwa ajili ya mazingira na pia imetoa Walimu 10 wanajeshi ambao wanafundisha shuleni hapo. Katika Mwaka wa Fedha 2018/2019, Serikali imependekeza shule hiyo itengewe shilingi milioni 230 ili kujenga maabara za sayansi mbili, jengo la utawala, bwalo na nyumba za Walimu endapo Bunge litaridhia.