Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 12 2018-04-04

Name

Dr. Joseph Kizito Mhagama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Madaba

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA aliuliza:-
Idadi ya watu nchini inazidi kuongezeka, ongezeko hili linaenda sambamba na ongezeko la mahitaji ikiwemo ardhi kwa ajili ya kilimo na ufugaji.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwajengea uwezo wakulima na wafugaji ili waendeshe shughuli zao katika maeneo madogo lakini kwa tija kubwa na kuwaondolea adha wanazozipata?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. GEORGE J. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama, Mbunge wa Madaba kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali huwajengea uwezo wakulima na wafugaji nchini kupitia elimu na ushauri wa kitaalam ambao hutolewa na Maafisa Ugani walioko kwenye Kata na Vijiji vya Halmashauri zote nchini. Hadi Desemba, 2017 tunao Maafisa Ugani 13,532. Kati ya hao Maafisa Ugani 8,232 ni wa kilimo cha mazao, 4,283 ni wa mifugo, 493 ni wa uvuvi na 524 ni wa ushirika.
Elimu ya kilimo na ufugaji bora hutolewa kupitia mashamba darasa 11,213 nchi nzima kwa wakulima na wafugaji wakubwa na wadogo, vikundi vya ushirika vya miradi ya umwagiliaji kwa njia ya mitaro na njia ya matone (drip irrigation) na vikundi vya ushirika vya ufugaji wa kisasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia awamu ya pili ya Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo itakayoanza kutekelezwa mwaka ujao 2018/2019 Serikali inaandaa mradi wa kilimo cha kutumia vitalu nyumba (green house) utakaotekelezwa kwa kila halmashauri kujenga vitalu nyumba visivyopungua viwili ili kusambaza teknolojia mpya ya kilimo yenye uwezo mkubwa wa kuzalisha shehena ya mazao mengi katika eneo dogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati mingine ni pamoja na kufanya sensa mahsusi ya kuwatambua wakulima wadogo na wakubwa, kuwasajili, kujua uwezo wao na kujua mahitaji yao ya mbegu, mbolea na madawa. Zoezi hilo limeanza na mazao ya kahawa, tumbaku, korosho, chai na pamba kwa mazao ya biashara; pamoja na mazao ya mahindi, mpunga, ngano na muhogo kwa upande wa mazao ya chakula. Takwimu hizo zitasaidia utekelezaji wa mikakati ya kuongeza uzalishaji kwa kuhakikisha pembejeo za kilimo zinawafikia wakulima mapema ili zitumike kwa wakati stahiki wa kilimo kwa lengo la kuongeza tija.