Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 46 2018-04-10

Name

Cecil David Mwambe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ndanda

Primary Question

MHE. CECIL D. MWAMBE aliuliza:-
Bwawa la Lukuledi ambalo huhudumia Kata za Lukuledi, Mpanyani na Chikinja ni muhimu sana kwa wananchi.
Je, Serikali itafanya lini ukarabati wa bwawa hilo kwa sababu kiwango cha maji kinapungua kwa kujaa mchanga?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil David Mwambe, Mbunge wa Jimbo la Ndanda, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali kupitia Wakala wa Uchimbaji Visima na Mabwawa (DDCA) inaendelea na kazi ya usanifu wa kina wa miundombinu ya Bwawa la Lukuledi lililojengwa mwaka 1954 ambalo ukarabati wake utakapokamilika litahudumia wananchi wapatao 11,544 kwenye vijiji vya Lukuledi A, Lukuledi B, Mraushi, Mkolopola, Ndomoni na Naipanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, usanifu huo unahusisha mabwawa mengine mawili yenye uwezo wa kuhudumia wananchi 15,746. Mabwawa hayo ni Bwawa la Mihima litakalohudumia vijiji vya Mihima, Muungano na Mpanyani na Bwawa la Chingulungulu litakalohudumia vijiji vya Chingulungulu, Namatutwe na Namalembo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la usanifu huo ni kubaini gharama zitakazohitajika kukarabati mabwawa hayo matatu yenye uwezo wa kuzalisha na kusambaza huduma ya maji kwa wananchi wapatao 27,290.