Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 7 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 62 2018-04-11

Name

Mussa Ramadhani Sima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Mjini

Primary Question

MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza:-
Tunatambua kuwa michezo duniani kote imekuwa chanzo cha mapato na kuinua uchumi wa Taifa husika, lakini nchini Tanzania michezo hususan soka imebaki kuwa burudani tu.
(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuinua Soka la Tanzania?
(b) Je, kuna mahusiano gani kati ya Serikali na TFF
katika kuimarisha soka la Tanzania kuanzia ngazi ya Wilaya?
(c) Je, Shirikisho la Mpira wa Tanzania (TFF) linapata fedha za ruzuku kiasi gani toka FIFA na Wadhamini kama TBL na Serengeti Breweries?

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Ramadhan Sima, Mbunge wa Singida Mjini, kama ifuatavyo:-
a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika kuhakikisha kuwa michezo ikiwepo soka inaimarika nchini, imeendelea kuendesha mashindano mbalimbali ya michezo mashuleni kitaifa ikiwepo UMISETA pamoja na UMITASHUMTA ili kuibua vipaji mapema na imeteua shule 56, mbili kwa kila mkoa hadi tatu kwa kila mkoa ili ziwe shule za michezo kwa ajili ya kukuza na kuendeleza vipaji vya michezo ikiwepo mchezo wa soka.
Aidha, Serikali kupitia Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya, imeendelea kutoa mafunzo ya muda mfupi na mafunzo ya muda mrefu kwa wakufunzi wa michezo mbalimbali ukiwepo mchezo wa mpira wa miguu.
b) Mheshimiwa Mwenyekiti, TFF, vyama vya michezo pamoja na mashirikisho mengine ya michezo vimesajiliwa na kufanya kazi chini ya Sheria ya Baraza la Michezo (BMT) Na. 12 ya mwaka 1967 na marekebisho yake ya mwaka 1971. Aidha, TFF inaendelea na uboreshaji wa viwanja vya soka nchini, mfano ni viwanja vya Kaitaba na Nyamagana mkoani Mwanza. Vilevile TFF inatoa msaada wa kiufundi katika viwanja mbalimbali ili kuhakikisha kwamba viwanja vinakuwa katika ubora unaotakiwa. Wizara yangu inaunga mkono programu mbalimbai za TFF katika kukuza mchezo wa mpira wa miguu wilayani na mikoani zikiwemo programu mpya kabisa za grass root pamoja na programu ya live your goals kwa wanawake ambazo zilizinduliwa Mkoani Kigoma Februari, 2018. BMT nayo inaendelea kusimamia utekelezaji wa Katiba, Kanuni na Sheria zinazosimamia michezo mbalimbali nchini.
c) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mapato ya TFF; kwanza TFF ina udhamini wa miaka minne (2015-2018) kutoka FIFA kwenye programu ya FIFA Forward ambayo hutoa kiasi cha dola za Kimarekani milioni 1.25 kwa mwaka ambapo kati ya hizo dola za Kimarekani 750,000 hutumika kwa ajili miradi ya maendeleo na dola za Kimarekani 500,000 hutumika kwa ajili ya gharama za kuendeshea ofisi, timu za Taifa pamoja na ligi. Fedha hizi za maendeleo hazikuwahi kutolewa na FIFA tangu mwaka 2015, hivyo, TFF wanatarajia kupokea kiasi fedha cha dola za Kimarekani milioni tatu kwa ajili ya kutekeleza miradi husika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, TFF iliingia mkataba na Kampuni ya Bia ya TBL mwaka 2013-2017 kwa thamani ya Dola za Kimarekani milioni 10 kwa ajili ya Timu ya Taifa ambap kwa sasa mkataba huo umeshamalizika. Hivyo, TFF imeingia mkataba wa ufadhili na Kampuni ya Bia ya Serengeti wa miaka mitatu (2017-2019) wenye thamani ya shilingi milioni 700 kwa ajili ya timu ya Taifa ya wanaume na shilingi milioni 450 kwa ajili ya ligi kuu ya wanawake nchini.