Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 12 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 95 2018-04-18

Name

Salma Rashid Kikwete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mchinga

Primary Question

MHE. SALMA R. KIKWETE aliuliza:-
(a) Kwa kuwa elimu ni haki ya kila mtoto, je, Serikali inawasaidiaje watoto wenye usonji ili nao wapate elimu?
(b) Je, Walimu wanaofundisha watoto hao wanatosheleza kwa mujibu wa ikama?
(c) Kwa kuwa watoto hao wana mazingira tete, je, Walimu wao wana utaalam wa kutosha?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete, Mbunge wa Kuteuliwa, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, usonji ni ulemavu ambao huathiri mfumo wa mawasiliano katika ubongo, mahusiano na utambuzi. Wanafunzi wenye usonji wamekuwa wakifundishwa na Walimu watalaam wa ulemavu wa akili waliopatiwa mafunzo kazini. Hadi sasa tuna wanafunzi 1,416 wenye usonji na Walimu 157 walio katika shule 18 za msingi nchini. Walimu hao ni wachache na hawatoshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wapo Walimu waliopata taaluma hiyo kwenye Chuo cha Patandi, lakini hawako kwenye shule maalum, nasisitiza tena agizo langu nililolitoa kwenye Mkutano wa Kumi kwamba Halmashauri zote ziwahamishie Walimu hao kwenye shule zenye wanafunzi wenye ulemavu ikiwemo wenye usonji ifikapo mwezi wa Desemba, 2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utoaji wa elimu maalum nchini kwa wanafunzi wenye ulemavu wasioona, viziwi, albino, usonji, viziwi–wasioona, walemavu wa akili, walemavu wa viungo, uoni hafifu, wenye vipawa na vipaji pekee pamoja na wenye matatizo ya ujifunzaji utaendelea kupewa kipaumbele. Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia ikiwemo miundombinu, vifaa maalum kwa mahitaji maalum, kutoa mafunzo zaidi kwa Walimu pamoja na kugharamia kwa ujumla elimu msingi bila malipo kwa wanafunzi wote ikiwemo wenye mahitaji maalum.