Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 13 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 108 2018-04-19

Name

Andrew John Chenge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi

Primary Question

MHE. ANDREW J. CHENGE aliuliza:-
Katika miaka ya 1980 wanakijiji wa Kijiji cha Mwanchumu, Salaliya na Matongo walitoa maeneo yao kwa Serikali ili yatumike kwa shughuli za kilimo zilizokusudiwa na Gereza la Matongo lakini kwa sasa maeneo hayo hayatumiwi na Magereza kikamilifu.
Je, Serikali ipo tayari kurejesha eneo hilo ambalo halitumiki kikamilifu kwa wananchi wa vijiji hivyo?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Andrew John Chenge, Mbunge wa Bariadi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Gereza la Matongo liko Mkoani Simiyu katika Wilaya ya Bariadi na lina ukubwa wa hekari 2472.62. Gereza hili lilianzishwa mwaka 1975 kwa kuchukua eneo lililokuwa la Mbunge wa zamani wa eneo hilo, Marehemu Edward Ng’wani ambapo alifidiwa eneo hilo kwa kupewa eneo lingine na Serikali. Aidha, wananchi wa Vijiji vya Mwanchumu, Salaliya kwa asili ni wahamiaji kutoka maeneo mengine na siyo wenyeji wa Matongo.
Mheshimiwa Spika, ikumbukwe kuwa Serikali iko kwenye mpango wa kuboresha kilimo kupitia Jeshi la Magereza kwa kuliwezesha kuzalisha chakula cha kutosheleza kulisha wafungwa na mahabusu. Eneo la Gereza la Matongo lipo kwenye orodha ya maeneo yaliyopewa kipaumbele katika kilimo cha mahindi, alizeti, pamba, ufugaji wa nyuki na mifugo pamoja na upandaji wa miti na uhifadhi wa mazingira.
Mheshimiwa Spika, Serikali ilitwa eneo hilo ili kuwezesha Magereza kuendeleza shughuli za urekebishaji wafungwa kwa kutumia kilimo cha ufugaji ambapo mazao mbalimbali ya kilimo hustawi. Kwa sasa eneo hilo limeshapimwa na taratibu za kufuatilia upatikanaji wa hati unaendelea.
Mheshimiwa Spika, kutokana na eneo hilo kuwa kwenye mpango mkakati wa Jeshi la Magereza wa kujitosheleza kwa chakula na shughuli nyingine, Serikali haina mpango wa kulirejesha eneo hilo kwa vijiji tajwa.