Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 21 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 173 2018-05-03

Name

John Wegesa Heche

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. MWITA M. WAITARA (K.n.y MHE. JOHN W. HECHE) aliuliza:-
Mazingira ya ufundishaji kwa Walimu walio wengi nchini ikiwemo Wilaya ya Tarime yamekuwa siyo rafiki, ambapo Walimu wamekuwa wakibebeshwa mzigo wa gharama za vifaa vya kufundishia kama maandalio ya somo, chaki na kadhalika:-
Je, matumizi haya yatarekebishwaje katika mfumo huu wa elimu bure ulioanzishwa na Serikali ya Awamu ya Tano.

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kwa ruhusa yako, nimpe pole Mheshimiwa John Heche na wote ambao wamefiwa, Serikali ipo pamoja nao katika misiba hiyo.
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa John Wegesa Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, ambapo marekebisho yake madogo naomba yaingie katika Hansard kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kupitia Waraka wa Elimu Na.5 wa mwaka 2015, uliotoa mwongozo wa Serikali kuhusu Elimu Msingi bila malipo, majukumu ya Serikali, jamii, wazazi, walezi, wakuu wa shule, Kamati au Bodi za shule, yamefafanuliwa vizuri sana kwenye Waraka huo. Miongoni mwa majukumu ya Serikali ni kutoa ruzuku ya uendeshaji wa shule, inayogharamia chakula kwa wanafunzi wa bweni, ununuzi wa vitabu vya kiada na ziada, vitambulisho, mitihani endelezi, mitihani ya Taifa, shughuli za michezo, maandalio ya somo, chaki na vifaa vingine. Hivyo siyo sahihi kwa Walimu kutumia fedha zao kugharamia maandalio ya somo na vifaa kama chaki.
Mheshimiwa Spika, nawaagiza Wakurugenzi wote wa Halmashauri, Maafisa Elimu wote wa ngazi zote na Walimu Wakuu kusimamia vizuri Mpango wa Utoaji Elimu Msingi bila malipo kama ulivyofafanuliwa katika waraka nilioutaja, kuanzia sasa Walimu wasikubali kubebeshwa mizigo ya gharama isiyowahusu.