Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 30 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 256 2018-05-16

Name

Maryam Salum Msabaha

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARYAM SALUM MSABAHA aliuliza:-
Bagamoyo ni mji mkongwe wenye vivutio vya kitalii kama ilivyo miji mingine nchini kama vile Zanzibar, Kilwa na Mapango ya Amboni, Tanga.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha vituo vya kitalii nchini ikiwemo Bagamoyo ili kupata wageni wengi zaidi na kukuza pato la Taifa?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Salum Msabaha, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Bagamoyo ni moja ya miji mikongwe katika historia ya utamaduni na maendeleo ya Tanzania ukiwa kando kando ya Bahari ya Hindi. Bagamoyo ni moja ya vituo vya Malikale ambavyo ni mojawapo ya vivutio vya utalii hususani wa utamaduni hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, vivutio hivyo havitumiki ipasavyo katika kukuza utalii kutokana na changamoto mbalimbali ambazo ni ufinyu wa bajeti, ukosefu wa huduma muhimu kwa watalii, kutofikika, kuchakaa kwa vioneshwa na kutotangazwa ipasavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia changamoto hizo, Wizara imeandaa mkakati wa kuvitambua na kuvitangaza vivutio vyote nchini ukiwemo Mji wa Bagamoyo. Mpango huu unalenga kushirikisha mashirika yaliyo chini ya Wizara, yaani Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS).
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, vivutio vya malikale vilivyo Bagamoyo ni miongoni mwa maeneo yatakayoendelezwa kwa ushirikano na mashirika hayo. Aidha, vivutio vyote vya utalii nchini vitaendelea kutangazwa kupitia taasisi zinazohusika ikiwemo Bodi ya Utalii Tanzania (TTB). Kazi zitakazotekelezwa na mashirika hayo ni pamoja na kuweka huduma muhimu kwa watalii, kuboresha miundombinu ya vituo hususani majengo na barabara ili kuwezesha kufikika kwa urahisi na kuwa na mwonekano unaovutia; kujenga vituo vya kumbukumbu na taarifa pale ambapo vinahitajika, kuboresha vioneshwa na kuvitangaza na kuhamasisha wawekezaji wa hoteli, michezo na vivutio vingine vya watalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mkakati huu, Wizara itaendelea kusimamia majukumu yote ya uhifadhi, utafiti na kuandaa taarifa zitakazosaidia kuboresha na kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini, kwa kutoa elimu kwa umma juu ya uhifadhi na matumizi endelevu ya malikale na maliasili za nchi yetu. (Makofi)