Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 3 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 35 2018-09-06

Name

Jaku Hashim Ayoub

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

House of Representatives

Primary Question

MHE. JAKU HASHIM AYOUB aliuliza:-
Benki Kuu ya Tanzania (BOT) inalo jukumu la kuzisimamia benki nyingine hapa nchini pamoja na kulinda haki za wateja wa benki za biashara. Kwa zaidi ya miaka miwili sasa Benki ya FBME imefungwa kwa sababu ya ukiukwaji wa sheria za kifedha na mpaka sasa jambo hilo halijapatiwa ufumbuzi.
(a) Je, ni sababu gani inayofanya benki hiyo isiwalipe wateja wake haki zao au amana zao?
(b) Je, Serikali haioni kuwa BOT imeshindwa kutimiza wajibu wake wa kuzisimamia benki nyingine na kuwafanya wananchi kukosa imani na mifumo ya kibenki inayorudisha nyuma utaratibu wa kuhifadhi fedha?
(c) Je, Serikali haioni kuwa tunakosa mapato ambayo yangetusaidia kwa ajili ya maendeleo ya nchi?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jaku Hashim Ayoub lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa kifungu cha 11(3)(i), 41(a), 58(2) na 61(1) vya Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006 Benki Kuu ya Tanzania ilisimamisha shughuli zote za Benki ya FBME na kufuta leseni ya biashara, kuiweka chini ya ufilisi na kuiteua Bodi ya Bima ya Amana kama mfilisi tarehe 8 Mei, 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hatua hiyo, jukumu la kuwalipa wateja wa Benki ya FBME haki au Amana zao kisheria lipo mikononi mwa Bodi ya Bima ya Amana na siyo Benki ya FBME. Malipo ya fidia au amana kwa wateja yamechukua muda mrefu kwa sababu ya taratibu za kisheria zinazotakiwa kuzingatiwa katika zoezi zima la ufilisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, zoezi la kulipa fidia kwa wateja waliokuwa na amana katika Benki ya FBME kwa mujibu wa sheria lilianza mwezi Novemba, 2017 na bado linaendelea. Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Julai, 2018 asilimia 60 ya wateja wa benki hiyo walikuwa wamelipwa fidia ya amana na Bodi ya Bima ya Amana.
b) Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa majukumu ya msingi ya Benki Kuu ni kusimamia utendaji wa kila siku wa taasisi za kifedha hususan benki. Katika kutekeleza jukumu hili, Benki Kuu kuchukua hatua kuinusuru benki husika ikiwemo kusimamia uendeshaji wa shughuli za benki au kuifutia leseni mara tu inapobaini viashiria vya kufilisika au upungufu mkubwa wa ukwasi kinyume na matakwa ya Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006 na Kanuni zake. Lengo la kufanya hivyo ni kulinda walaji, amana za wateja na kujenga imani ya wananchi kuhusu mifumo ya benki na utaratibu wa kuhifadhi fedha kwenye mabenki.
Pili, Benki Kuu husimamia taratibu zote za ufilisi kwa taasisi itakayofutiwa leseni na kuhakikisha kuwa wateja wanapata fidia kwa mujibu wa sheria. Kwa kuzingatia sheria na kanuni zilizopo, majukumu haya mawili yanaendelea kutekelezwa na kusimamiwa vizuri na Benki Kuu. Hivyo basi, siyo kweli kwamba Benki Kuu imeshindwa kuzisimamia taasisi za fedha na benki na hivyo kuwafanya wananchi kukosa imani na mifumo ya kifedha nchini
c) Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ukweli kuwa Taifa linakosa mapato ambayo yangesaidia kuleta maendeleo, ni lazima kuzingatia matakwa ya kisheria, kanuni na taratibu zilizopo ili zoezi hili liweze kufanyika kwa ufanisi. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, zoezi la ufilisi linafanyika kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za ufilisi wa kampuni. Napenda kulihakikishia Bunge lako tukufu kwamba, Mfilisi wa Benki kwa kushirikiana na Benki Kuu anafanya juhudi za kukusanya madeni pamoja na fedha za benki zilizopo kwenye benki nyingine nje ya nchi ili kulipa amana za wateja kwa kadri itakavyowezekana.