Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 5 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 57 2018-09-10

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itapitia upya Sera ya Michezo nchini?

Name

Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Answer

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako naomba kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo, nitoe pole kwa ndugu, jamaa na marafiki wa Watanzania wenzetu 11 waliopoteza maisha na wengine 15 waliojeruhiwa katika ajali nyingine mbaya ya Mlima Igawilo, Mkoani Mbeya, Mungu aziweke roho zao pema peponi.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kufa ni wajibu na maisha lazima yaendelee, niruhusu vilevile nielezee kidogo yaliyotokea Uingereza usiku wa kuamkia jana kwa Mtanzania mwenzetu Hassan Mwakinyo wa Tanga kwa ushindi mnono alioupata huko Birmingham, Uingereza, baada ya kumchakaza mwanamasumbwi nyota wa Uingereza Sam Eggington katika raundi ya pili tu kati ya raundi 10. (Makofi)
Kabla ya pambano hili kufanyika bondia wa Uingereza alikuwa bondia namba nane kwa ubora duniani kati ya Mabondia 1,852 wakati Hassan Mwakinya alikuwa ni Bondia wa 174 na sasa hivi kutokana na matokeo haya Hassan ni wa 16 duniani, ni bondia bora wa kwanza Barani Afrika na bondia wa kwanza Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya haya, naomba sasa kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Sera ya Maendeleo ya Michezo inayotumika sasa hivi ni ya mwaka 1995, ni dhahiri kuwa katika miaka 23 ya sera tuliyonayo sasa tasnia ya michezo imepitia mabadiliko mengi yanayoleta hitaji la mabadiliko kisera kama vile michezo kuwa chanzo kikubwa cha ajira ya uhakika duniani, kuibuka kwa michezo ya kulipwa, ongezeko la mahitaji ya shule na vyuo mahsusi vya michezo mbalimbali kwa lengo la kulea vipaji toka udogoni kwa wavulana na wasichana, ongezeko la hitaji la viwanja vizuri na vya kutosha ngazi za shule za msingi, sekondari, vyuo, sehemu za kazi na makazi kwa lengo la kuibua viipaji na kupunguza gharama za matibabu kwa magonjwa yanayotokana na mwili kukosa mazoezi, ongezeko kubwa la mahitaji ya vifaa mbalimbali vya michezo na umuhimu wa kujenga uwezo wa ndani kuzalisha vifaa hivyo.
Mheshimiwa Spika, ni kutokana na hali hii halisi Wizara ilianzisha mwaka jana zoezi la kuipitia upya Sera ya Maendeleo ya Michezo ya mwaka 1995, zoezi ambalo limehusisha ukusanyaji wa maoni kutoka kwa wadau mbalimbali ndani na nje ya nchi. Uandaaji wa rasimu kamili ya Sera mpya ya Maendeleo ya Michezo umefikia hatua za mwisho na ni matarajio ya Wizara kukamilisha zoezi hili ndani ya muda mfupi ujao.
Mheshimiwa Spika, kupatikana kwa sera mpya kutaleta tija na kutuwezesha kuleta mabadiliko chanya katika tasnia ya michezo nchini ikiwa ni pamoja na kutuwezesha kubadili sheria iliyoanzisha Baraza la Michezo la Taifa (BMT) ili iweze kuleta ufanisi katika uendeshaji wa michezo nchini, ikiwa ni pamoja na kuainisha vyanzo rasmi na endelevu vya mapato katika maendeleo ya michezo nchini.