Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 70 2018-09-11

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-
Katika Mji Mdogo wa Mbalizi kuna ardhi ya ukubwa wa zaidi ya ekari 5,000 iliyotengwa kwa ajili ya Tanganyika Packers ambayo haijaendelezwa kwa zaidi ya miaka 30 iliyopita.
(a) Je, ni lini Serikali itawarudishia wananchi wa Mji Mdogo wa Mbalizi eneo hilo kwa lengo la kuliendeleza kwa kubadili matumizi kutokana na kukua kwa kasi kubwa kwa Mji wa Mbalizi?
(b) Pamoja na kubadili matumizi ya ardhi hiyo, je, Serikali ina mpango gani kwa wananchi wanaotumia ardhi hiyo hasa ikizingatiwa kuwa wengi wao hawakupewa fidia yoyote?

Name

Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, shamba namba 760 lenye hekta 102.4 na shamba namba 761 lenye hekta 1985.4 yaliyoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ambayo kwa pamoja yana ukubwa wa hekta 2,087.8 sawa na ekari 5,219.5 ni mali ya Serikali. Mwaka 1974 Serikali ilijenga Kiwanda cha Kusindika Nyama cha Tanganyika Packers kwenye shamba namba 760 na shamba namba 761 lilikuwa maalum kwa ajili ya kupumzisha mifugo na kuilisha vizuri kabla ya kuchinjwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya uzalishaji kiwandani kusimama kutokana na changamoto kadhaa za kiuendeshaji na kiuchumi, baadhi ya wananchi walivamia maeneo ya mashamba hayo na tarehe 4/3/2016, Halmashauri ya Wilaya iliomba kwa Msajili wa Hazina kubadilisha matumizi ya eneo hilo kuwa makazi na huduma nyingine. Ombi hilo lilikataliwa kwa kuwa nia ya Serikali kuliendeleza eneo hilo kama eneo la viwanda haijawahi kubadilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ndiyo maana ili kuona kuwa haki inatendeka Serikali ilifungua kesi Namba 1 ya mwaka 2015 Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya dhidi ya wavamizi ambayo ilihukumiwa tarehe 20/2/2018 kwa Serikali kupewa haki ya kuendeleza eneo lake. Taratibu za kisheria za kuwaondoa wavamizi ili eneo hilo litumike kama ilivyokusudiwa zitakamilishwa hivi karibuni. Serikali haijawahi na haina mpango wa kubadili matumizi ya eneo hilo, kwani kufanya hivyo kwa maeneo kama hayo ni kukwamisha juhudi za kujenga Tanzania ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa kumbukumbu zilizopo wananchi waliokuwa wanastahili fidia kwa mujibu wa sheria wote walilipwa.