Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 11 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 90 2016-05-03

Name

Juma Othman Hija

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tumbatu

Primary Question

MHE. JUMA OTHMAN HIJA aliuliza:-
Katika Jimbo la Tumbatu kumekuwa na matukio ya uvunjifu wa amani kwa wananchi wanaoishi katika kisiwa hicho na katika hali ya namna hiyo inaporipotiwa kwa Jeshi la Polisi inakuwa tabu kwenda kwa haraka kwenye eneo husika kwa sababu kadhaa ikiwemo ya ukosefu wa usafiri:-
Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga Kituo cha Polisi katika kisiwa hicho na kuwapatia usafiri wa uhakika kwa kuzingatia jiografia ya maeneo hayo?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Othman Hija, Mbunge wa Tumbatu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yapo matukio ya kihalifu yanayoripotiwa kutokea katika Kisiwa cha Tumbatu. Jeshi la Polisi linafanya jitihada za kukabiliana na uhalifu kwa kutoa huduma za ulinzi na usalama katika maeneo ya Kisiwa cha Tumbatu kwa kila siku kuwapeleka Askari wa doria ili kuimarisha ulinzi. Kwa sasa lipo boti lenye uwezo wa kubeba Askari 10, iwapo uwezo wa kifedha ukiongezeka hitaji letu ni kupata boti kubwa la mwendo kasi lenye uwezo wa kubeba Askari zaidi ya 10.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaona haja ya kuwepo Kituo cha Polisi katika eneo hilo, ili kusogeza huduma za ulinzi na usalama na hali halisi ya kisiwa hicho kilichozungukwa na bahari na uwepo wa matukio ya uhalifu. Katika kutekeleza hilo tayari Serikali imepata kiwanja na makisio ya ujenzi wa kituo hicho yanaendelea. Aidha, Serikali kupitia Bunge lako Tukufu inapenda kuhamasisha wadau werevu na wananchi, akiwemo Mheshimiwa Mbunge, kutoa msaada wa hali na mali katika ujenzi wa kituo hiki.