Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 47 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 402 2018-06-08

Name

Ally Abdulla Ally Saleh

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Malindi

Primary Question

MHE. ALLY SALEH ALLY aliuliza:-
Mchezo wa chess au sataranji unakuza akili, uwezo wa kufikiri na kufanya maamuzi na ni mzuri sana kwa vijana ambao wanakulia na kuingia hasa katika masomo ya sayansi na ufundi.
(a) Je, mchezo huo umejikita kiasi gani hapa nchini hadi sasa?
(b) Je, kunaweza kuwa na mipango ya kufanya juu ya mchezo huo kuwa wa lazima na sehemu ya mtaala kwa kuiga hasa nchi za Ulaya ya Mashariki?

Name

Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Answer

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Saleh Ally, Mbunge wa Malindi, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na Mheshimiwa Ally Saleh Ally kama ilivyo kwa michezo mingine, mchezo wa chess au saratanji unakuza akili, hilo tunakubali, uwezo wa kufikiri na kufanya maamuzi. Hata hivyo, mchezo huu bado haujaenea sana hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuhakikisha kuwa michezo ikiwemo mchezo wa chess inaimarika nchini. Wizara, kupitia Baraza la Michezo la Taifa na Chuo cha Maendeleo ya Michezo - Malya kwa kushirikiana na wadau wa mchezo huu itaangalia uwezekano wa kutoa mafunzo kwa lengo la kuueneza mchezo huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Serikali itaendelea kuhamasisha wananchi katika maeneo mbalimbali kushiriki katika mchezo huu kama inavyofanya katika michezo mingine ili kuueneza mchezo huu kwa manufaa ya jamii kwa ujumla, kwani tayari umeshasajiliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwa sasa Serikali haina mpango wa kuufanya mchezo huu kuwa wa lazima kufundishwa kwenye shule kwa kuuingiza kwenye mitaala yetu. Pia suala la kuingiza mchezo kuwa sehemu ya mtaala linahusisha wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na Wizara mbalimbali na hasa baada ya kujiridhisha kwa kufanya tafiti za kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema hapo awali, Waheshimiwa Wabunge na wadau wote wa Sekta ya Michezo waendelee kutoa ushirikiano wa kutosha ili kuhakikisha kuwa michezo, ikiwemo mchezo wa chess inasonga mbele. (Makofi)