Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 48 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 410 2018-06-11

Name

Masoud Abdalla Salim

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtambile

Primary Question

MHE. MASOUD A. SALIM aliuliza:-
Kwa mujibu wa Ibara ya 141(2) ya Katiba ya Nchi, Deni la Taifa maana yake ni deni lenyewe, faida inayolipwa juu ya deni hilo, fedha zilizowekwa akiba kwa ajili ya kulipa deni hilo polepole na gharama zote zinazoambatana na deni hilo:-
a) Je, Deni la Taifa hadi swali hili linajibiwa ni kiasi gani?
b) Je, mchanganuo wa fedha zilizowekwa akiba kwa ajili ya kulipa deni hilo ukoje?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kabla ya kuanza kujibu swali hili, naomba nikushukuru sana kwa safari yako muhimu uliyoifanya Jimboni kwangu Kondoa juzi tarehe 9 Juni, 2018. Mwenyezi Mungu akubariki na akupe afya njema sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Masoud Abdallah Salim, Mbunge wa Mtambile, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, hadi kufikia 30 Aprili, 2018, Deni la Taifa lilikuwa Dola za Kimarekani milioni 26,161.02 sawa na shilingi bilioni 59,480.74.
(b) Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Deni la Taifa linajumuisha deni la Serikali na deni la sekta binafsi, Serikali inawajibika kufanya malipo ya deni la Serikali na si Deni la Taifa kwa ujumla wake. Aidha, fedha kwa ajili ya malipo ya Deni la Serikali inatengwa kwa kuzingatia taratibu za kawaida za kibajeti kupitia Fungu 22. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali ilitenga kiasi cha shilingi bilioni 1,262.42 kwa ajili ya malipo ya deni la ndani na shilingi bilioni
685.06 kwa ajili ya malipo ya deni la nje. Hivyo basi, hakuna fedha iliyowekwa akiba kwenye mfuko maalum kwa ajili ya kulipia deni la Taifa.