Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 49 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 419 2018-06-12

Name

Rhoda Edward Kunchela

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Katavi

Primary Question

MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-
a) Je, ni lini Serikali itatatua mgogoro wa ardhi kati ya Hifadhi na wananchi katika Kata ya Kapalamsenga, Isengule na Ikola?
b) Kwa kuwa migogoro hiyo imechukua muda mrefu bila suluhu hivyo kusababisha usumbufu na hasara kwa wananchi; Je, Serikali haioni kuwa migogoro hiyo imesababisha umaskini mkubwa kwa wananchi kushindwa kuendeleza shughuli za kiuchumi kwenye maeneno yao hivyo ifanye haraka kutafuta ufumbuzi?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Kapalamsenga, Isengule na Ikola zipo katika Wilaya ya Tanganyika na zinajumuisha maeneo ya ushoroba wa wanyamapori ujulikanayo kama Katavi – Mahale. Ushoroba huu ni njia kuu ya wanyamapori kutoka Hifadhi ya Taifa Katavi kwenda Hifadhi ya Taifa Mahale. Kutokana na wanyamapori hususani tembo kupita katika maeneo hayo, wenyeji wanautambua ushoroba husika kama “Tembo na Mwana.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ushoroba huu kufahamika kwa baadhi ya wananchi kulikuwa na mkanganyiko kuhusu eneo sahihi la (mipaka), yaani mipaka ya mapito ya wanyamapori na hii inatokana na baadhi ya wananchi na hasa wahamiaji na wafugaji kutoka mikoa ya jirani, kuvamia na kuharibu maeneo ya mapito ya wanyamapori bila kufuata taratibu na kujichukulia ardhi kiholela.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutafuta ufumbuzi wa migongano hii iliyopo juu ya matumizi ya ardhi, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika ilichukua hatua mbalimbali kama ifuatavyo:-
• Kuhakikisha kuwa mipaka ya ushoroba inajulikana kwa wananchi kwa kutenga na kuainisha maeneo kwa ajili ya uhifadhi wa wanyamapori kama vile Sokwe. Sokwe hao wanapatikana katika Kata za Kapalamsenga, Ikola, Isengule, Mwese na Kasekese hasa katika safu za milima ya Mwansisi na Mgengebe.
• Kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi ya vijiji na kutunga sheria ndogo za usimamizi wake kwa mwaka wa fedha 2015/2016 na 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa vijiji vyote vilivyopo katika Kata ya Kapalamsenga, Ikola na Isengule vimeshafanyiwa mpango shirikishi wa matumizi bora ya ardhi. Pia, eneo la ushoroba wa wanyamapori limebainishwa na kutengwa hivyo kuondoa mkanganyiko uliokuwepo awali. Aidha, kwa kutumia Kanuni ya usimamizi wa shoroba na maeneo ya mtawanyiko zimeshaandaliwa (GN 123 ya mwaka 2018).
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango wa kutafuta suluhu ya kudumu kwa wananchi katika vijiji vyote vinavyopitiwa na shoroba za wanyamapori, vinavyopakana na maeneo ya hifadhi na vyanzo vya maji ili kuondoa migongano inayohusiana na umiliki wa matumizi ya ardhi. Hivyo, tunawaomba wananchi wote kuheshimu mipaka ya matumizi bora ya ardhi pamoja na kanuni mpya za ushoroba.