Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 43 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 365 2018-06-04

Name

Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Primary Question

MHE. QAMBALO W. QULWI aliuliza:-
Matukio ya Wanyamapori kutoka nje ya Hifadhi ya Ngorongoro kwenda katika vijiji vinavyopakana na hifadhi hiyo Wilayani Karatu na kuharibu mazao ya wananchi na kujeruhi watu yamekuwa yakijirudia mara kwa mara:-
• Je, ni nini mkakati wa Serikali kuwadhibiti wanyama hao ili wabaki katika maeneo waliyotengewa;
• Fidia/Kifuta jasho kinachotolewa pindi wanyama wanapofanya uharibifu ni kidogo sana na imepitwa na wakati. Je, ni lini Serikali italeta marekebisho ya kifuta jasho, ili kuendana na mazingira ya sasa?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Qambalo Willy Qulwi, Mbunge wa Karatu, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, uharibifu wa mali na maisha ya binadamu kutokana na wanyamapori wakali na waharibifu unajitokeza katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwa ni pamoja na maeneo yanayozunguka Hifadhi ya Ngorongoro. Katika Eneo la Ngorongoro uharibifu unajitokeza zaidi katika maeneo ya mashamba na makazi ya wananchi wanaoishi pembezoni mwa hifadhi hiyo.
Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Karatu inakabiliana na changamoto ya uharibifu wa mali na maisha ya binadamu kwa kufanya doria za pamoja. Aidha, Mamlaka ya Ngorongoro ina vituo vitano katika maeneo ya Kilimatembo, Elewana, Nitini, Bonde la Faru na Masamburai kwa ajili ya kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu, vilevile magari mawili yamenunuliwa kwa ajili ya madhumuni hayohayo.
Mheshimiwa Spika, juhudi nyingine zinazofanyika ni kuendelea kutoa elimu ya namna ya kujihami na kudhibiti wanyamapori, hususan tembo. Elimu hiyo, inahusisha matumizi ya pilipili, mafuta machafu na mizinga ya nyuki kuzunguka mashamba kama njia ya kufukuza tembo.
Mheshimiwa Spika, fedha za kifuta jasho na kifuta machozi hazitolewi kama fidia bali hutolewa kwa ajili ya kuwafariji wananchi walioathirika na wanyamapori wakali na waharibifu. Hivyo, fedha hizo kuwa ni kidogo na hazilingani na hali halisi ya uharibifu.
Mheshimiwa Spika, kulingana na wingi wa matukio pamoja na ufinyu wa bajeti Serikali imeamua kupitia Kanuni za Kifuta Machozi na Kifuta jasho ili kuondoa changamoto zilizopo kiutendaji.