Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 53 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 451 2018-06-19

Name

Marwa Ryoba Chacha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Serengeti

Primary Question

MHE. MARWA R. CHACHA aliuliza:-
Kumekuwepo na tabia ya askari wa SENAPA kuwakamata wananchi ndani ya hifadhi na wakati mwingine wasipouawa huwapeleka mbali na Mahakama za Wilaya ya Serengeti.
(a) Je, ni lini vitendo vya mauaji ya watu wanaozunguka Hifadhi ya Serengeti vitakoma?
(b) Je, ni lini askari wa SENAPA wataacha kuwapeleka watuhumiwa waliokamatwa ndani ya hifadhi nje ya Mahakama za Wilaya?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha, Mbunge wa Serengeti, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Askari wa Hifadhi ya Taifa ya Serengeti wanafanya kazi kwa mujibu wa sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali iliyopo. Ni kweli kwamba baadhi ya wananchi wamekuwa wakikamatwa na kufanya shughuli au kuingia kwenye hifadhi bila ya kufuata taratibu zilizopo. Wengi wamekuwa wakijihusisha na ujangili ndani ya hifadhi. Kwa msingi huo, Askari wa Hifadhi huwakamata watuhumiwa wote na kuwafikisha katika Jeshi la Polisi na hatimaye Mahakamani kwa hatua zaidi. Jumla ya kesi 437 zimefunguliwa na zipo katika hatua mbalimbali za usikilizaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti imepakana na Wilaya nane tofauti. Mtuhumiwa anapokamatwa ndani ya hifadhi, anapelekwa katika Kituo cha Polisi kilicho jirani kwa hatua zaidi. Baadhi ya watuhumiwa wamekuwa na tabia ya kufanya uhalifu kwa kufuata mienendo ya wanyamapori wahamao. Kwa mfano, kati ya mwezi Mei na Juni ya kila mwaka, wanyama wengi wanahamia maeneo ya Kusini na Magharibi mwa Hifadhi ambapo kiutawala yako Wilaya ya Bariadi na Bunda.
Hivyo baadhi ya watuhumiwa kutoka Wilaya ya Serengeti huenda katika Wilaya nyingine kufanya ujangili wa wanyamapori ambapo kwa kipindi hicho hawapatikani kirahisi katika aneo la Wilaya zao. Kutokana na hali hiyo, watuhumiwa wamekuwa wakikamatwa na kushitakiwa katika Mahakama za eneo au Wilaya waliyokamatwa wakifanya uhalifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema wananchi wakazingatia taratibu zote za Hifadhi na niwaase wananchi hao kuachana na ujangili ili kuepuka adhabu hizo na kuwataka washirikiane na Serikali kulinda hifadhi za Taifa.