Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 9 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 74 2018-04-13

Name

Julius Kalanga Laizer

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Monduli

Primary Question

MHE. CECILIA D. PARESSO – (K.n.y. MHE. JULIUS K. LAIZER) aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatoa fidia stahiki kwa wananchi ambao mazao yao yaliharibiwa na wanyamapori tangu mwaka 2010 hadi 2017 katika maeneo ya Mswakini, Makuyuni, Naiti, Mbuyuni, Lokisale na maeneo mengine Wilayani Monduli?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Julius Kalanga Laizer, Mbunge wa Monduli, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wanyamapori wakali na waharibifu ni kubwa na linajitokeza katika zaidi ya Wilaya 80 nchini. Uharibifu mkubwa wa mali na madhara kwa binadamu vikiwemo vifo husababishwa na tembo, mamba, nyati, kiboko, simba na fisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uharibifu unaotokana na wanyamapori kwa sehemu kubwa unasababishwa na ongezeko la watu na shughuli zao ambazo mara nyingine zinafanyika katika maeneo yaliyo karibu na hifadhi au kwenye mapito ya wanyamapori. Aidha, mabadiliko ya tabianchi yamechangia pia katika kubadili mzunguko na mtawanyiko wa asili wa wanyamapori wakati wa kutafuta mahitaji muhimu, hususani chakula na maji. Hali hiyo kwa ujumla wake imeongeza ukubwa wa tatizo la muingiliano wa binadamu na wanyamapori na kusababisha uwepo wa matukio mengi ya uharibifu wa mali na madhara kwa binadamu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuzingatia changamoto zilizopo, Wizara yangu kwa kushirikiana na halmashauri ya Wilaya ya Monduli, inaendelea kukabiliana na tatizo la wanyamapori wakali na waharibifu kwa kufanya doria za udhibiti wa wanyamapori hao katika maeneo mbalimbali ya Wilaya hiyo kulingana na taarifa za uharibifu zinazowasilishwa na wananchi husika. Aidha, Wizara itaendelea kutoa elimu ya njia mbadala ya udhibiti wa tembo na wanyamapori wengine katika Wilaya ya Monduli na maeneo mengine, mathalani matumizi ya uzio wa kamba zilizopakwa mchanganyiko wa pilipili na oili chafu, matumizi ya matofali ya kinyesi cha tembo kilichochanganywa na pilipili na mizinga ya nyuki kuzunguka mashamba ambayo tembo huogopa na kuondoka maeneo hayo. Sanjari na hayo, Wizara itaendelea kuelimisha wananchi kuhusu njia bora za kujikinga na wanyamapori wengine kwa kuhimiza ujenzi wa nyumba bora na imara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Kanuni za Kifuta jasho na Machozi za Mwaka 2011, Serikali imekuwa ikitoa fedha kidogo za kuwafariji wananchi kwa kuwalipa kifuta jasho kwa uharibifu wa mali (mazao na mifugo) na kifuta machozi kwa madhara kwa binadamu (vifo na majeruhi). Katika kutekeleza mpango huo, jumla ya shilingi 48,015,000 zililipwa kwa wananchi 251 wa vijiji vya Wilaya ya Monduli waliokidhi vigezo vya kulipwa kuanzia mwaka 2010 hadi mwezi Aprili, 2018.