Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 1 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 7 2019-01-29

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:-

Halmashauri ya Busokelo ina maporomoko ya maji (waterfalls) maeneo mbalimbali na jotoardhi (geothermal):-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kutumia maporomoko hayo ya maji (waterfalls) na jotoardhi (geothermal) kuweza kuzalisha umeme ili kupunguza changamoto ya umeme nchini?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Fredy Atupele Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli katika Halmashauri ya Busokelo kuna maeneo yenye maporomoko ya maji yanayoungana na maporomoko yaliyoko Wilaya ya Makete katika Mto Rumakali. Upembuzi yakinifu katika maeneo hayo ulifanywa na Serikali mwaka 1998 kwa ushirikiano na Serikali za Norway na Sweden.

Mheshimiwa Spika, kulingana na upembuzi yakinifu huo maporomoko ya Mto Rumakali yanaweza kuzalisha umeme wa MW 222. Kwa sasa TANESCO inaendelea na kazi ya kuhuisha upembuzi yakinifu kupitia ufadhili wa Benki ya Dunia kabla ya kuanza hatua za utekelezaji. Utekelezaji wa mradi utaanza Aprili, 2020 na kukamilika Desemba, 2023.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kusimamia utekelezaji wa miradi ya jotoardhi ya Ngozi, Kiejo-Mbaka Mkoani Mbeya na Songwe Mkoani Songwe. Miradi hii yote imefikia hatua ya uchorongaji visima vya majaribio ili kuhakiki kiasi na ubora wa rasilimali ya jotoardhi katika maeneo hayo. Aidha, TANESCO kupitia Kampuni Tanzu ya Jotoardhi inaendelea na utafiti wa vyanzo vya umeme wa jotoardhi katika eneo la Mbaka katika Halmashauri ya Busokelo.

Mheshimiwa Spika, matokeo ya utafiti huo yataonyesha hali halisi ya uwezo wa kuzalisha umeme kwa nguvu za jotoardhi itakayopatikana katika eneo husika. Kazi ya utafiti na uchorongaji huo inatarajiwa kukamilika mwaka 2022.