Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:- Halmashauri ya Busokelo ina maporomoko ya maji (waterfalls) maeneo mbalimbali na jotoardhi (geothermal):- Je, Serikali haioni umuhimu wa kutumia maporomoko hayo ya maji (waterfalls) na jotoardhi (geothermal) kuweza kuzalisha umeme ili kupunguza changamoto ya umeme nchini?

Supplementary Question 1

MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri na nimpongeze pia Waziri mwenye dhamana kwa namna ambavyo waliweza kutembelea Jimbo langu la Busokelo na kufanya mikutano mingi na wananchi wale.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa mradi huu umechukua muda mrefu, ni zaidi ya miaka 21 sasa tangu upembuzi yakinifu ufanyike, je, Serikali haioni umuhimu wa kuharakisha mradi huu ili ifikapo 2022 uweze kukamilika badala ya mwaka ambao Mheshimiwa Waziri ameusema?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa umeme wa jotoardhi ni umeme endelevu kwa maana ya renewable na tumeona katika nchi yetu na tafiti zimeonyesha tunaweza kupata megawatts zaidi ya 5,000 kwa vyanzo vyote ambavyo vimeainishwa kwa nchi nzima ya Tanzania. Je, Serikali ina mpango gani wa kuviendeleza vyanzo hivyo ili Tanzania ifikapo 2025 iwe ni nchi ya uchumi wa kati?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake ya awali ambayo ametoa ufafanuzi mzuri sana katika mradi wa kuzalisha umeme wa jotoardhi. Sambamba na shukrani kwa Naibu Waziri wangu, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge Mwakibete kwa anavyofuatilia masuala ya rasilimali ya jotoardhi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, katika maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwakibete, la kwanza amesema imechukua muda mrefu kufanya utafiti kwa takribani miaka 21. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge lakini niwape taarifa Watanzania kwamba katika hatua za utekelezaji wa upembuzi yakinifu, mradi ambao umeenda kwa kasi katika miradi ya jotoardhi ni pamoja na mradi huu wa Ngozi ambao utatuzalishia MW 20.

Mheshimiwa Spika, kwa kawaida miradi ya jotoardhi, upembuzi yakinifu huchukua takribani miaka 25 - 40. Kwa hatua hii, ndiyo maana tunasema tumekwenda kwa kasi na tuna matumaini ya kukamilisha mapema mwaka uliotajwa wa 2023 tutapata MW 30.

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, nchi yetu ina rasilimali nyingi sana na madini ya jotoardhi (geothermal) kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge. Rasilimali tuliyonayo inaweza kutuzalishia megawatt zaidi ya 5,000, ingawa kwa sasa tathmini zinavyoonyesha tunaweza tukaanza kuzalisha MW 200 kwa kuanzia ifikapo miaka mitano ijayo. Tutaanza na MW 30 ambayo itatoka kwenye eneo la Ngozi kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, lakini nieleze tu kidogo, niwapongeze sana wananchi wa Mbozi na wananchi wengine wa maeneo yanayozunguka mradi huu kwa sababu wametupa ushirikiano mkubwa wa kufanya tathmini. Hivi sasa tunaendelea na kufanya tathmini ya maeneo mengine mengi nchini ikiwemo eneo la Majimoto kule Katavi ambayo nayo itatuzalishia megawatt za uhakika. Kwenye mradi wetu tutapata MW 5,000 miaka kumi au ishirini ijayo lakini itakuwa ni umeme wa uhakika ambao uta-stabilize sana upatikanaji wa umeme hapa nchini. Ahsanteni sana.