Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 4 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 46 2019-02-01

Name

Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Primary Question

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA aliuliza:-

Msitu wa Nyera – Kipelele ni miongoni mwa misitu ya asili iliyopo Wilaya ya Liwale. Serikali imekuwa ikiandaa taratibu za uvunaji wa mazao ya msitu huo.

(a) Je, taratibu hizo zitakamilika lini?

(b) Je, Serikali imepata manufaa gani kutokana na uhifadhi wa msitu huo?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zuberi Mohamed Kuchauka, Mbunge wa Liwale, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Msitu wa Nyera – Kipelele ni hifadhi ya msitu ulio chini ya umiliki wa usimamizi wa Serikali Kuu (Wakala wa Misitu wa Huduma Tanzania). Misitu hiyo ipo katika Wilaya ya Liwale, Mkoa wa Lindi, Msitu wa Kipelele ulitengwa kuwa hifadhi ya Serikali Kuu katika Tangazo la Serikali Na. 79 la mwaka 1956 ukiwa na eneo la hekta 98,423. Msitu huo umezungukwa na vijiji tisa, ambavyo ni Kichonda, Nyera, Kimambi, Mtawatawa, Kitogoro, Litou, Legezamwenda, Kipelele na Naujombo.

Mheshimiwa Naibu Spika, taratibu za kuandaa uvunaji wa mazao ya msitu katika msitu huo zimekamilika mwaka 2018, baada ya kuandaliwa kwa mpango wa usimamizi wa msitu (Management Plan) na mpango wa uvunaji (Harvesting Plan). Kwa mujibu wa mpango wa usimamizi, kiasi cha hekta 59,053 katika msitu huo zina miti ya kuweza kuvunwa. Aidha, miti ya ujazo 19,970 zimepangwa kuvunwa kuanzia mwaka
2019/2010 kwa kufuata mwongozo wa uvunaji wa mazao ya misitu.

Mheshimiwa Spika, manufaa yanayopatikana kutokana na uhifadhi wa msitu huo ni makazi ya wanyamapori aina tofauti wakiwemo tembo, uboreshaji wa mifumo ya kiikolojia ikiwemo hifadhi ya hewa ya ukaa. Aidha, ni vyanzo vya maji katika Vijiji vya Mtawatawa, Kitogoro, Legeza mwendo, Kipelele na vilevile hifadhi hiyo ni chanzo kikubwa cha mapato ya Serikali.