Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 6 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 54 2019-02-04

Name

Kemirembe Rose Julius Lwota

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. KEMILEMBE J. LWOTA) aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kumalizia ujenzi wa maboma ya Zahanati yaliyoanzishwa kwa juhudi za wananchi pamoja na kuyawekea vifaa tiba?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kemilembe Julius Lwota, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mwaka 2017 Serikali ilifanya tathmini kubaini idadi ya maboma nchi nzima ambayo ni Vituo vya Afya, Zahanati na nyumba za watumishi na kubaini kuwa kuna maboma 1,845 ambayo yanahitaji jumla ya shilingi bilioni 934 ili kukamilishwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali iliona ni vigumu kukamilisha maboma hayo kwa pamoja kutokana na upatikanaji wa fedha. Hivyo, ikabuni mkakati wa kujenga na kukarabati Vituo vya Afya 350 nchini vilivyochaguliwa kwa kutumia vigezo ambavyo ni uhitaji mkubwa wa huduma za dharura na upasuaji wa akina mama wajawazito, sababu za kijiografia na umbali mrefu ambao wananchi wanatembea kupata huduma za dharura.

Mheshimiwa Spika, vilevile, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2017/2018 na 2018/2019, jumla ya maboma 207, Vituo vya Afya sita, Zahanati 191 na nyumba kumi yalikamilishwa kwa fedha kutoka Mradi wa Mfuko wa Pamoja wa Afya na Mapato ya Ndani ya Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kuzielekeza Halmashauri zote nchini kutenga fedha kwenye makusanyo yake ya ndani na kuendelea kushirikisha wananchi na wadau wengine wa maendeleo kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa maboma wakati Serikali ikiendelea kutafuta fedha za ujenzi na ukarabati wa maboma hayo.