Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 10 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 113 2019-02-08

Name

Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Primary Question

MHE. JEROME D. BWANAUSI aliuliza:-

Wananchi wengi wameendelea kupoteza maisha na kujeruhiwa na mamba katika Mto Ruvuma:-

Je, ni lini wananchi walioathirika na mamba katika Vijiji vya Miesi Utimbe, Naliongolo, Mtolya, Geuza na Mchoti watalipwa fidia zao kwa mujibu wa sheria?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jerome Dismas Bwanausi, Mbunge wa Jimbo la Lulindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imekuwa ikilipa kifuta machozi kwa wananchi ambao wameshambuliwa na wanyamapori wakali kwa mujibu wa Kanuni za Kifuta Jasho na Machozi za Mwaka 2011. Kuanzia mwaka 2013 mpaka 2018 jumla ya Sh.37,300,000/= zimelipwa kwa wananchi 65 waliopatwa na madhara kutokana na wanyamapori wakali, hususan mamba, katika Wilaya ya Masasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kupunguza matukio ya wananchi kuendelea kupoteza maisha na kujeruhiwa na mamba, hasa wanapokwenda kuchota maji mtoni, Wizara kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA) imechimba visima vya maji tisa katika vijiji vilivyo kandokando ya Mto Ruvuma. Vijiji hivyo, ni chipingo, Nalimbudi, Chikolopora, Maparawe, Mbangala, Geuza na Mkowo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, katika kukabiliana na changamoto za athari zilizosababishwa na mamba, mwezi Julai, 2016, Wizara ilitoa kibali kwa Kampuni ya Ontour Tanzania Limited ambayo ilivuna mamba nane katika Mto Ruvuma na kupunguza kwa kiasi kikubwa matukio ya wananchi kujeruhiwa na kuuawa na mamba. Mfano katika kipindi cha Februari, 2018 mpaka sasa Wizara yetu haijapokea taarifa yoyote kuhusu wananchi waliouawa na kujeruhiwa na mamba katika eneo hilo. Ahsante.