Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Primary Question

MHE. JEROME D. BWANAUSI aliuliza:- Wananchi wengi wameendelea kupoteza maisha na kujeruhiwa na mamba katika Mto Ruvuma:- Je, ni lini wananchi walioathirika na mamba katika Vijiji vya Miesi Utimbe, Naliongolo, Mtolya, Geuza na Mchoti watalipwa fidia zao kwa mujibu wa sheria?

Supplementary Question 1

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri. Kwa kuwa, bado wananchi wa jimbo langu hasa wanaoishi kandokando mwa Mto Ruvuma wameendelea kupoteza maisha na kupoteza viungo vyao kwa kasi kubwa sana. Je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari sasa kuendelea kutimiza makubaliano yetu ya kuchimba visima katika vijiji sita vilivyobaki ili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata unafuu wa kuathirika na suala la mamba?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali langu la pili, Mheshimiwa Waziri anakiri kwamba, lipo tatizo kubwa, lakini tatizo lililopo ni kwamba, wenzetu wa TAWIRI ambao wanatoa vibali vya kuvuna mamba wanatoa idadi ndogo sana ya vibali, kama alivyoeleza ni mamba tisa, lakini takwimu zinaonesha katika eneo hilo pekee lina mamba zaidi ya 300. Je, yupo tayari kutoa vibali zaidi ili wananchi hao waweze kuondokana na tatizo hili kwa kuvuna mamba?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Bwanausi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nitumie nafasi hii kumpongeza kwa namna anavyofuatilia haki za wananchi wake walioshambuliwa na mamba. Kuhusu swali lake la kwanza amesema tatizo la wananchi kushambuliwa na mamba bado linaendelea na palikuwa na makubaliano na Wizara yangu kupitia TAWA ya kuchimba visima. Kama makubaliano hayo yalifanyika na Serikali haina kipingamizi, nitawaelekeza TAWA kuhakikisha kwamba, makubaliano hayo yanatimizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali lake la pili, ni kweli kwamba, kabla ya kuvuna mamba Shirika letu ya Utafiti la TAWIRI huwa linafanya utafiti kujiridhisha na idadi sahihi na kama idadi hiyo ni tishio katika eneo husika. Nitawaelekeza pia, TAWIRI wafanye upya utafiti na iwapo itathibitika kwamba, idadi ya mamba waliopo sasa ni tishio tutatoa tena kibali cha kuvuna mamba hao kupunguza athari kwa wananchi.

Name

Pauline Philipo Gekul

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. JEROME D. BWANAUSI aliuliza:- Wananchi wengi wameendelea kupoteza maisha na kujeruhiwa na mamba katika Mto Ruvuma:- Je, ni lini wananchi walioathirika na mamba katika Vijiji vya Miesi Utimbe, Naliongolo, Mtolya, Geuza na Mchoti watalipwa fidia zao kwa mujibu wa sheria?

Supplementary Question 2

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuunipa nafasi ili niulize swali moja la nyongeza. Sisi Babati tuna ziwa ambalo lina viboko na wavuvi wanapokwenda kufanya kazi zao wamekuwa wakiuawa na viboko hao, lakini hakuna fidia. Tulipohoji pia, hata kwa Wataalam wa Halmashauri wanadai kwamba, wavuvi wanakuwa wamefuata viboko hivyo, hawastahili fidia. Naomba nifahamu Wizara inatusaidiaje ili kujua kwamba, wavuvi wa Babati na wananchi wale wanastahili fidia au la?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gekul, Mbunge wa Babati, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yapo matukio ya wananchi wa Babati kushambuliwa wao wenyewe na viboko, lakini pia mashamba yao kuharibiwa na mamba. Kimsingi wananchi wale wanastahili kupata fidia iwapo shambulio hilo litatokea nje ya eneo la makazi ya viboko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu ya sheria viboko hawa wanapokuwa katika eneo lao makazi
wanapomshambulia mtu inakuwa ni mtu ndiye aliyekwenda kuwavamia katika eneo lao. Nimhakikishie Mheshimiwa Gekul, iwapo kuna wananchi ambao malalamiko yao yapo na walishambuliwa nje ya eneo ambalo ni makazi ya viboko, Wizara yetu itachukuwa hatua ikiwa ni pamoja na kuagiza pia watu wa TAWIRI kufanya utafiti na kuona idadi ya mamba hao kama wanaleta tishio ili waweze kuvunwa.