Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 10 2019-04-03

Name

Mgeni Jadi Kadika

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM (K.n.y. MHE. MGENI JADI KADIKA) aliuliza:-

Katika baadhi ya maeneo hapa nchini ikiwemo Dodoma wapo watoto ambao hutoa huduma ya kubeba mizigo na kupewa ujira mdogo. Kutokana na kufanya kazi hizo ni wazi wanakosa haki za msingi kama elimu na malezi bora.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuondoa tatizo hilo?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mgeni Jadi Kadika, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, huduma za ulinzi wa mtoto zinatekelezwa kupitia Sheria ya Mtoto Na. 21 ya mwaka 2009. Katika kusimamia utekelezaji wa Sheria hiyo, Mamlaka za Serikali za Mitaa zinatekeleza Mpango Kazi wa Taifa wa kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto ulioanza kutekelezwa kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018 hadi 2021/ 2022. Tathmini imebaini kuwa watoto wengi wanaojihusisha na kazi za kubeba mizigo masokoni ni matokeo ya umasikini uliokithiri kwa baadhi ya kaya, kuondokewa na wazazi wao kwa maambukizi ya UKIMWI, migogoro ya ndoa na ukatili dhidi ya watoto.

Mheshimiwa Spika, mkakati unaotekelezwa na Serikali ni kutoa elimu kwa jamii kuhusu haki za msingi za mtoto kupata elimu na malezi bora. Aidha, utoaji wa elimu bila malipo umetoa fursa kwa watoto wengi wenye umri wa kwenda shule kuandikishwa kuanza elimu ya awali kupitia mfumo rasmi na mfumo usio rasmi. Vilevile, mradi wa TASAF umewezesha kuzitambua kaya za watoto walio katika mazingira hatarishi na kuzisaidia kiuchumi ili ziweze kumudu mahitaji ya kaya zao kwa kuwapatia watoto mahitaji ya msingi ikiwemo elimu na afya.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatoa wito kwa wazazi kutimiza wajibu wao wa kuwalea na kuwatunza watoto ikiwemo kuwapa fursa ya elimu. Aidha, jamii inao wajibu wa kushirkiana na wazazi kuwatunza na kuwalinda watoto ambao ni Taifa la kesho kwa kutowatumikisha katika kazi ambazo haziendani na umri wao. Serikali haitasita kuchukua hatua kwa vitendo vyovyote vya unyanyasaji wa watoto vinavyokiuka Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009.