Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 8 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 62 2019-04-11

Name

Richard Phillip Mbogo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. RICHARD P. MBOGO aliuliza:-

Mabadiliko ya Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa Sura 290 yameleta nafuu sana kwa wakulima, lakini wakati huo huo Halmashauri za Wilaya zenye wakulima wadogo zimeathirika kimapato na kusababisha kushindwa kutatua kero za wananchi kwa wakati.

(a) Je, Serikali inaweza kuangalia upya suala la utaoji ruzuku za maendeleo?

(b) Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo imeathirika kwa kiwango kikubwa: Je, Serikali ipo tayari kuipatia ruzuku ili kutoa huduma za elimu na afya?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura ya 290 imefanyiwa marekebisho na Bunge Mwezi Juni, 2017 kwa kupunguza kiwango cha ushuru wa mazao kutoka asilimia tano hadi asilimia tatu kwa mazao ya chakula na biashara. Hata hivyo, Mamlaka za Serikali za Mitaa zimeendelea kubuni vyanzo vipya vya mapato na kuimarisha makusanyo katika vyanzo vilivyopo ili kuongeza mapato na kuboresha utaoji huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na mikakati hiyo, mapato ya ndani ya Halmashauri yameendelea kuongezeka kila mwaka. Mfano, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Halmashauri ziliidhinishiwa kukusanya shilingi bilioni 687 na zilikusanya shilingi bilioni 553.39 sawa na asilimia 81. Katika mwaka wa fedha 2018/2019, Halmashauri zimeidhinishiwa kukusanya shilingi bilioni 735.58 hadi Februari, 2019 zimekusanywa shilingi bilioni 401 sawa na asilimia 55. Aidha, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Halmashauri zimekadiria kukusanya shilingi bilioni 765.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali halisi kwa ujumla inaonyesha makusanyo ya Halmashauri yameendelea kuongezeka pamoja na kupungua kwa ushuru wa mazao kutokana na Halmashauri kubuni vyanzo mbalimbali vya mapato na vyanzo mbadala. Ofisi ya Rais, TAMISEMI itaendelea kuzisimamia Halmashauri katika ukusanyaji wa mapato ya ndani ili kuimarisha makusanyo na kupunguza utegemezi kutoka Serikali kuu.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi mwaka 2019, Serikali imepeleka kiasi cha shilingi milioni 416 kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kwa ajili ya kugharamia Elimu Msingi Bila Malipo, shilingi milioni 250 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma 20 ya shule za sekondari na shilingi 411 kwa ajili ya ununuzi wa dawa, vitendanishi na vifaa tiba. Serikali itaendelea kuongeza utoaji wa ruzuku kwa mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.