Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 14 Works, Transport and Communication Ofisi ya Rais TAMISEMI. 110 2016-05-06

Name

Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Primary Question

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE aliuliza:-
Moja ya matukio makubwa ya kihistoria katika nchi yetu ni vita ya Majimaji iliyopiganwa kati ya mwaka 1905 – 1907 kati ya Watanganyika na Wajerumani. Pamoja na kufahamu kwamba vita hivyo vilienea katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu, lakini vilianza katika Kijiji cha Nandete, Wilaya ya Kilwa; Serikali inaonesha jitihada mbalimbali ya kuienzi historia hiyo, ikiwa ni pamoja na kujenga mnara katika Kijiji hicho:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza barabara ya kutoka Njianne hadi Nandete kwa kiwango cha lami ili kulifanya eneo hilo la kihistoria kufikiwa kwa urahisi na kuliongezea umaarufu kwa kutembelewa na watalii hususani wa kutoka Ujerumani jambo ambalo litaiongezea mapato Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa na Taifa kwa ujumla.

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vedasto Edgar Ngombale, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa kujenga barabara ya lami kwenda eneo hili la kihistoria ni la msingi, lakini kwa sasa wakati Serikali inajenga barabara kuu zote nchini kwa kiwango cha lami hasa zikiunganisha Makao Makuu ya Mikoa yote. Hata hivyo, Serikali imekuwa ikitenga bajeti ya fedha kwa ajili ya matengenezo ili kuifanya ipitike wakati wote.
Kupitia Wakala wa barabara Mkoa wa Lindi, katika mwaka wa fedha 2015/2016, zilitengwa shilingi milioni 58.8 kwa ajili ya matengenezo ya kawaida kilomita 43 na matengenezo ya muda maalum kwa kiwango cha changarawe urefu wa kilomita sita, kwa jumla ya gharama ya shilingi milioni 192.3. Matengenezo ya barabara hii yameanza chini ya Mkandarasi Ungando Contractors Company wa Kibiti – Rufiji. Aidha, katika bajeti ya mwaka 2016/2017, barabara hii iko katika mpango wa kufanyiwa matengenezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kilomita 10 zinazohudumiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, katika mwaka 2015/2016, zimetengwa shilingi milioni 70 ambazo zitatumika kwa ajili ya matengenezo ya muda maalum kwa urefu wa kilomita nane. Katika mwaka wa fedha 2016/2017, zimetengwa shilingi milioni 967.6 ambazo zitatumika kwa ajili ya matengenezo ya barabara katika Wilaya ya Kilwa.