Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Primary Question

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE aliuliza:- Moja ya matukio makubwa ya kihistoria katika nchi yetu ni vita ya Majimaji iliyopiganwa kati ya mwaka 1905 – 1907 kati ya Watanganyika na Wajerumani. Pamoja na kufahamu kwamba vita hivyo vilienea katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu, lakini vilianza katika Kijiji cha Nandete, Wilaya ya Kilwa; Serikali inaonesha jitihada mbalimbali ya kuienzi historia hiyo, ikiwa ni pamoja na kujenga mnara katika Kijiji hicho:- Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza barabara ya kutoka Njianne hadi Nandete kwa kiwango cha lami ili kulifanya eneo hilo la kihistoria kufikiwa kwa urahisi na kuliongezea umaarufu kwa kutembelewa na watalii hususani wa kutoka Ujerumani jambo ambalo litaiongezea mapato Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa na Taifa kwa ujumla.

Supplementary Question 1

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa vita ya Majimaji au harakati za awali za kudai uhuru wa Tanganyika zilitokana na chokochoko na misingi imara ya kukataa kuonewa na kudai uhuru kulikofanywa na majemedari wetu wakati wa vita vya Majimaji. Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga barabara hii ili kuwawezesha Watanzania kwenda katika eneo hilo wakajifunze namna gani nchi yetu ilivyojengwa katika misingi ya kudai haki? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kwa kuwa barabara hii haipitiki kabisa Serikali ina mpango gani wa kuweka lami katika sehemu korofi kwa mfano mlima Ndundu, Mlima Ngoge pale Chumo, Mlima Kinywanyu na Mlima Karapina pale Kipatimu?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi kwamba umuhimu wa barabara hii na Mheshimiwa Mbunge amesema kwamba sehemu hii ndiyo chemichemi za harakati ya ukombozi wa nchi yetu. Naomba nikiri kwamba, kuna maeneo mengi sana ya kijiografia ambayo wakati wa uhuru kama Tanzania tulipokuwa tunaenda katika mchakato walishiriki kwa kiwango kikubwa sana katika kufanikisha uhuru wa nchi yetu, nawapongeza sana ndugu zetu wa Kilwa katika hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakiri wazi kwamba kwa sababu umuhimu wa barabara hii kama nilivyosema awali katika jibu langu, tukirejea tena marejeo ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi, lengo lake kubwa ni kuhakikisha wananchi wanafikiwa wa maeneo mbalimbali. Mheshimiwa Ngombale tutafanya juhudi siyo hapo Kilwa tu, isipokuwa maeneo mbalimbali. Ndiyo maana Ofisi ya Rais, TAMISEMI ilikuwa ikifanya mikakati katika maeneo mbalimbali, tulianza hasa katika miji tumeenda katika halmashauri, lengo letu ni kwamba maeneo mbalimbali yaweze kufikika chini ya miradi yetu ambayo sasa hivi tuna mradi wa TSP Project ambayo inahusisha ujenzi wa miundombinu ya barabara za lami katika maeneo mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hili litakuwa katika mpango wetu, mkakati mpana wa kuhakikisha Halmashauri nyingi zinafikiwa na haya ni mambo ambayo tunayafikiria, ndiyo maana hata ukiangalia bajeti yetu ya mwaka huu tuna bajeti takribani ya bilioni 43 kwa ajili ya kuondoa vikwazo, lakini bilioni zaidi ya 200 kwa ajili ya kuhakikisha Halmashauri ziweze kufikiwa vizuri. Kwa hiyo, ni mambo ambayo Serikali yetu inayaangalia na ndani ya miaka mitano tuna imani tutafanya mambo makubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lile la kuhusu sasa vile vipande korofi ikiwezekana viwekewe lami na najua Halmashauri ya Kilwa jinsi gani jiografia yake ilivyo na wakati mwingine malori yanashindwa kupanda. Tutawaelekeza wenzetu wa TANROAD ambao tunashirikiana nao kwa karibu zaidi na barabara takribani kilomita 48 zinahudumiwa na TANROAD, tutahakikisha Serikali inayapa kipaumbele yale maeneo korofi ambayo mvua ikinyesha barabara hazipitiki kwa kuyafikiria kwa jicho la karibu zaidi.

Name

Pauline Philipo Gekul

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE aliuliza:- Moja ya matukio makubwa ya kihistoria katika nchi yetu ni vita ya Majimaji iliyopiganwa kati ya mwaka 1905 – 1907 kati ya Watanganyika na Wajerumani. Pamoja na kufahamu kwamba vita hivyo vilienea katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu, lakini vilianza katika Kijiji cha Nandete, Wilaya ya Kilwa; Serikali inaonesha jitihada mbalimbali ya kuienzi historia hiyo, ikiwa ni pamoja na kujenga mnara katika Kijiji hicho:- Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza barabara ya kutoka Njianne hadi Nandete kwa kiwango cha lami ili kulifanya eneo hilo la kihistoria kufikiwa kwa urahisi na kuliongezea umaarufu kwa kutembelewa na watalii hususani wa kutoka Ujerumani jambo ambalo litaiongezea mapato Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa na Taifa kwa ujumla.

Supplementary Question 2

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Pamoja na mikakati ya Serikali kujenga barabara za lami, lakini kuna ahadi ya Mheshimiwa Rais ambayo aliitoa katika maeneo yetu wakati anaomba kura, ya ujenzi wa barabara za lami. Katika Bunge hili tuliomba tupatiwe time frame kwamba ni muda gani hizi ahadi zinatekelezwa. Nataka kufahamu ni lini Mheshimiwa Waziri atatuletea ratiba ya ujenzi wa barabara hizo za lami kwa ahadi ya Rais ili tufuatilie kwa karibu ikiwemo Jimbo langu la Babati Mjini kilomita ishirini za lami?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ni lini, kifupi time frame ya ujenzi wa utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, imeainishwa ndani ya miaka mitano 2015-2020. Jukumu letu kubwa ni kuhakikisha ndani ya kipindi hiki zile ahadi ambazo tumeahidi kwa kadri ilani yetu ilivyojielekeza, tutajitahidi kwa kadri iwezekanavyo, ili mwisho wa siku tuone kwamba ilani yetu imetekelezwa kwa ajili ya kuwapatia wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania maendeleo ya kutosha na siyo Babati peke yake, isipokuwa kwa Tanzania nzima kwa mujibu wa Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi.