Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 11 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 97 2019-04-16

Name

Juma Othman Hija

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tumbatu

Primary Question

MHE. JUMA OTHMAN HIJA aliuliza:-

Thamani ya Shilingi ya Tanzania inaendelea kuporomoka kila siku, kuporomoka huko kunachangia kwa kiasi fulani ugumu wa maisha kwa wananchi wa kawaida katika kupanga mipango yao ya kimaisha:-

Je, Serikali ina mkakati gani ya kudhibiti mporomoko huo?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Othman Hija, Mbunge wa Tumbatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, thamani ya shilingi dhidi ya sarafu nyingine hutegemea nguvu za soko, yaani ugavi na mahitaji. Sababu za kushuka kwa thamani ya shilingi dhidi ya fedha za kigeni ni pamoja na tofauti ya mfumuko wa bei kati ya Tanzania na nchi wabia katika biashara, mauzo kidogo nje ya nchi, mahitaji makubwa ya kuagiza bidhaa na huduma kutoka nje; kupungua kwa misaada na mikopo kutoka nje; kuimarika kwa fedha za kigeni kutokana na kuimarika kwa uchumi wa nchi wabia katika biashara na kuzuka kwa biashara ya kuhisia na kuotea ya sarafu za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, sababu zote hizi hazikuwepo na hivyo thamani ya shilingi yetu dhidi ya Dola ya Marekani ilikuwa tulivu ikilinganishwa na sarafu nyingine dhidi ya Dola ya Marekani. Kwa mfano, thamani ya shilingi ilipungua kwa wastani wa 2% kwa mwaka 2017/2018 na 2016/2017 ikilinganishwa na wastani wa 22% mwaka 2015/2016.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiujumla shilingi ilikuwa imara ikilinganishwa na sarafu nyingine kama vile Franc ya Rwanda iliyopungua kwa wastani wa 5% na shilingi ya Uganda iliyoshuka kwa 3.8% katika kipindi kama hicho. Utulivu wa thamani ya shilingi ulitokana na utekelezaji thabiti wa sera za fedha na bajeti pamoja na kudhibiti mfumuko wa bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuimarisha utulivu wa thamani ya shilingi dhidi ya fedha za kigeni, Serikali inatekeleza mikakati ifuatayo:-

(i) Kuhakikisha kuwa ongezeko la ujazi wa fedha linaendana na ukuaji wa shughuli za uzalishaji;

(ii) Kuongeza uzalishaji wa bidhaa na huduma ndani ya nchi;

(iii) Kuongeza mauzo ya bidhaa na huduma nje ya nchi, na;

(iv) Kudhibiti hali ya wasiwasi katika soko la fedha za kigeni inayosababishwa na hisia pamoja na biashara ya kuotea ambapo Benki Kuu hununua na kuuza fedha za kigeni katika soko la jumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba jukumu la kuimarisha thamani ya shilingi ni shirikishi na pia lina wadau wengi na hivyo kila mmoja anahitajika kushiriki kwa nafasi yake ili kuleta mafanikio kwa nchi. Aidha, wadau wakuu ni Serikali pamoja na wananchi. Serikali ina majukumu makuu mawili:-

(i) Serikali kupitia Benki Kuu ina jukumu la kutekeleza na kusimamia Sera ya Fedha ili kudhibiti mfumuko wa bei, viwango vya kubadilisha fedha na ujazi wa fedha katika soko; na

(ii) Kuandaa na kusimamia sera thabiti za kibajeti, kuhakikisha nchi inakuwa na amani na utulivu na kujenga miundombinu wezeshi kwa ajili ya kuchochea uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, wananchi ambao ndio wawekezaji, wana jukumu la kuzalisha kwa wingi bidhaa na huduma mbalimbali hususan zile zinazoipatia nchi fedha za kigeni na/au zinazoipunguzia nchi mzigo wa mahitaji ya fedha za kigeni.