Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 21 Industries and Trade Wizara ya Viwanda , Biashara na Uwekezaji 170 2019-05-06

Name

Silafu Jumbe Maufi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SILAFU J. MAUFI aliuliza:-

Mkoa wa Rukwa umeanzishwa mwaka 1974 lakini hadi sasa hakuna viwanda vikubwa vilivyowekezwa na kuwekewa mikakati na Serikali na viwanda vilivyopo ni vya watu binafsi:-

(a) Je, Serikali ina mikakati gani ya kujenga viwanda au kupeleka wawekezaji ambao watajenga viwanda vikubwa Mkoa wa Rukwa ili kutoa ajira kwa vijana?

(b) Mazao yanayolimwa Mkoa wa Rukwa yanapewa bei kiholela na kufanya maisha ya wananchi kuwa magumu: Je, ni lini Serikali itaingia mkataba na viwanda vya uzalishaji?

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Silafu Jumbe Maufi, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Jukumu la Serikali katika ujenzi wa viwanda ni kuwepo mazingira rafiki na wezeshi na kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza na kufanya shughuli za kiuchumi ikiwemo kuzalisha na kufanya biashara. Msimamo huo wa kisera unaihusu mikoa na sekta zote za kiuchumi. Kwa msingi wa utaratibu huo wa kisera, Serikali imeelekeza nguvu zake katika kujenga na kuboresha miundombinu wezeshi na saidizi hususan umeme barabara, maji na mawasiliano. Aidha, katika kuhamasisha uwekezaji, Serikali imeitaka mikoa yote nchini kuandaa Taarifa za fursa za uwekezaji zilizopo (Regional Profiles) katika maeneo yake na kuvitangaza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pPia Serikali imeanzisha Mkakati wa zao moja Wilaya Moja (ODOP) ili kila Wilaya nchini ijielekeze katika kuendeleza angalau zao moja litakalovutia uwekezaji wa viwanda. Mkakati huu utasaidia kila Wilaya zikiwemo za Mkoa wa Rukwa kuwa na kiwanda angalau kimoja kinachotumia rasilimali zilizopo katika wilaya hizo. Hivyo, natoa wito kwa Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote tushirikiane kuainisha fursa zilizopo na kuzitangaza kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo cha mkataba hapa Tanzania kwa sasa kinatumika katika baadhi ya mazao yakiwemo miwa na tumbaku. Katika utaratibu huo wakulima hukubaliana na wanunuzi/viwanda kupewa baadhi ya huduma zikiwemo pembejeo kwa masharti ya kuwauzia mazao hayo na gharama za huduma au pembejeo hizo hukatwa wakati wa malipo. Katika utaratibu huo Serikali haihusiki moja kwa moja katika kuingia mikataba hiyo bali Maafisa Ugani huwasaidia wakulima kuangalia iwapo mikataba husika itakuwa na tija. Tunawahimiza wananchi kuwa makini wakati wa kuingia mikataba hiyo na wanunuzi. Aidha ili kupata nguvu ya soko, ni muhimu kuuza mazao kupita vyama vya ushirika.