Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 4 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 39 2020-01-31

Name

Godfrey William Mgimwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalenga

Primary Question

MHE. PAULINE P. GEKUL (K.n.y. MHE. GODFREY W. MGIMWA) aliuliza:-

Tatizo la ukosefu wa nyumba za Walimu kwenye maeneo mengi ya Jimbo la Kalenga kumesababisha Walimu kuhama na hivyo kudhoofisha ukuaji wa elimu kwa ujumla: -

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuisaidia Halmashauri ya Iringa Vijijini ili kuhakikisha inajenga nyumba za kutosha kwa Walimu?

(b) Mapato ya ndani ya Halmashauri hii hayatoshi kujenga nyumba za Walimu. Je, nini mkakati wa Serikali juu ya tatizo hili?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Kalenga lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali tayari imetoa Shilingi milioni 50 kwa ajili ya ukamilishaji wa ujenzi wa nyumba 2 za walimu katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa. Serikali inaendelea kutafuta fedha kupitia vyanzo mbalimbali kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya shule zikiwemo nyumba za walimu.

(b) Mheshimiwa Spika, Mkakati wa Serikali ni kuziwezesha halmashauri kuandaa maandiko ya miradi ya Kimkakati itakayoongeza mapato ya halmashauri ili kukidhi mahitaji yaliyopo ikiwemo ujenzi wa nyumba za walimu. Aidha, Halmashauri zimeelekezwa kubuni vyanzo vipya vya mapato na kuimarisha makusanyo ya mapato ya ndani na usimamizi wa vyanzo vilivyopo ahsante.