Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 7 Energy and Minerals Wizara ya Madini 93 2020-02-05

Name

Dr. Dalaly Peter Kafumu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igunga

Primary Question

MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU aliuliza:-

Madini ya Tanzanite yanapatikana nchini Tanzania pekee, juhudi za kufanya madini haya kuchimbwa na Watanzania pekee kwa Kanuni za Madini za mwaka 2004 na Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 hazijaweza kuzaa matunda:-

(a) Je, kwa nini Tanzania isiyatangaze madini ya Tanzanite kuwa ni Nyara za Taifa itayovunwa na Serikali pekee ili kuongeza manufaa ya kiuchumi kwa Taifa letu?

(b) Je, kwa nini Serikali isiende kujifunza nchini Zimbabwe kuona jinsi ilivyofanikiwa kuyafanya madini ya Almasi kuwa Nyara ya Serikali na hivyo kuleta manufaa makubwa sana kwa nchi hiyo?

Name

Doto Mashaka Biteko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukombe

Answer

WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Igunga, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inatambua upekee na umuhimu wa madini ya Tanzanite. Kwa muktadha huo, ilipelekea tarehe 20/9/2017 kuliamuru Jeshi la Wananchi wa Tanzania kujenga ukuta wenye urefu wa kilometa 24.5 kuzunguka eneo hilo. Lengo likiwa ni kudhibiti utoroshwaji wa madini ili kupata manufaa stahiki ya kiuchumi kwa mwananchi mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, eneo la Mirerani ambako Tanzanite inapatikana lilitangazwa kuwa eneo lililodhibitiwa (Mirerani Controlled Area) kwa GN 450 ya mwaka 2002. Lengo la hatua hiyo ni pamoja na kuthamini upekee na umuhimu wa madini hayo na kudhibiti upotevu wa mapato yanayotokana wa Madini ya Tanzanite ili kuongeza manufaa kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, Madini ya Tanzanite yanachimbwa na Watanzania katika Vitalu A, B, C na D-extension. Aidha, kitalu C kimekuwa kikichimbwa kwa ubia kati ya Shirika la STAMICO na Kampuni ya kigeni ya TanzaniteOne Mining Limited (TML). Hata hivyo, tarehe 23 Desemba 2019, STAMICO na TML waliachia eneo hilo na kupewa surrender certificate ya leseni yao na sasa eneo hilo limerudishwa kwenye usimamizi wa Serikali. Baada ya kuachiwa kwa eneo hilo, utaratibu maalum unaandaliwa wa namna bora ya kuligawa kwa kutoa leseni za uchimbaji wa kati kwa Watanzania wenye uwezo wa kulichimba na kuongeza mchango katika uchumi wa madini.

Mheshimiwa Spika, ushauri wa kuyafanya madini ya Tanzanite kuwa Nyara za Taifa na kwenda kujifunza katika nchi kama Zimbabwe, ushauri huo tunaupokea.