Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 7 Energy and Minerals Wizara ya Madini 94 2020-02-05

Name

Amb. Adadi Mohamed Rajabu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muheza

Primary Question

MHE. BALOZI ADADI M. RAJAB aliuliza:-

Katika Kata ya Mbomole maeneo ya Sakale Wilayani Muheza kuna madini ya dhahabu ambayo wananchi wamekuwa wakichimba bila vibali na hivyo kukamatwa kwa kuharibu chanzo cha maji cha Mto Zigi:-

(a) Je, ni lini Serikali itatuma watalaam ili kuweza kujua eneo hilo lina madini gani?

(b) Je, Serikali ipo tayari kuweka utaratibu mzuri ambao utahakikisha kuwa wachimbaji hao wanachimba eneo ambalo hawatasumbuliwa?

Name

Doto Mashaka Biteko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukombe

Answer

WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Adadi Mohamed Rajab, Mbunge wa Muheza, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tarehe 02/10/2018, Timu ya Wataalamu wa Madini, Mazingira na Maji kutoka Ofisi ya Tume ya Madini Tanga, Halmashauri ya Wilaya ya Muheza na Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira (NEMC) walitembelea na kukagua eneo la Sakale ili kuangalia athari za uchimbaji uliokuwa unafanywa na wachimbaji wadogo katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, baada ukaguzi wa timu hiyo, timu ya wataalam ilibaini uharibifu mkubwa wa mazingira uliofanywa katika vyanzo vya maji na Msitu wa Amani na hivyo shughuli za uchimbaji madini zilisitishwa katika eneo hilo ili kunusuru mazingira, vyanzo vya Maji na Msitu wa Amani katika Kata ya Mbomole.

Mheshimiwa Spika, tafiti mbalimbali za awali zilizofanywa na Taasisi ya Jiolojia Tanzania (GST) ilibaini uwepo wa madini ya dhahabu katika Vijiji vya Mindu, Tengeni, Segoma na Mbambara Muheza na Korogwe.

Mheshimiwa Spika, natoa wito kwa wachimbaji wadogo wa Kata ya Mbomole eneo la Sakale kuangalia maeneo mengine nje ya Bonde la Mto Zigi ili kufanya shughuli za uchimbaji.