Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 6 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 75 2019-11-12

Name

Ally Abdulla Ally Saleh

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Malindi

Primary Question

MHE. ALLY SALEH ALLY aliuliza:-

Moja ya misingi mikuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ni utawala bora, haki za binadamu na demokrasia sambamba na kukuza uchumi za Nchi sita Wanachama:-

(a) Je, hilo linatimizwa kwa kiasi gani ndani ya Jumuiya na Wanachama?

(b) Je, kuna mfumo gani wa kukosoana ndani ya Jumuiya katika eneo hilo?

Name

Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Saleh Ally, Mbunge wa Malindi, lenye vipengele (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 6 ya Mkataba wa Uanzishaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki imeainisha misingi mikuu ya kuzingatia ili kuiwezesha Jumuiya ya Afrika Mashariki na Nchi Wanachama kufikia malengo yake. Katika kutekeleza matakwa ya Ibara hiyo, nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zimegawanya madaraka katika mihimili mitatu yaani Bunge, Mahakama na Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Mihimili hii inajiendesha kwa kanuni na taratibu zake ambapo Wakuu wa Nchi kupitia Baraza la Mawaziri husimamia utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwemo maelekezo na maamuzi ya Wakuu wa Nchi; Bunge limepewa mamlaka ya kuwakilisha wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, kutunga sheria, kusimamia utekelezaji wa miradi na programu za Jumuiya pamoja na kupitisha bajeti ya Jumuiya; na Mahakama ina mamlaka ya kutafsiri Sheria za Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhamira hiyo ya kusimamia misingi mikuu ya Utawala Bora na Demokrasia ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Nchi Wanachama hupokezana Uenyekiti wa Jumuiya. Aidha, uendeshaji wa shughuli za Jumuiya hufuata vikao rasmi ambavyo ni shirikishi kuanzia ngazi ya Wataalam, Makatibu Wakuu, Baraza la Mawaziri na Wakuu wa Nchi, hivyo maamuzi yanayofikiwa ni yaliyokubalika na nchi zote sita (consensus). Mathalani, nchi hizo zimekubaliana kutuma waangalizi wa uchaguzi kwenye chaguzi kuu za nchi wanachama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Jumuiya ya Afrika Mashariki hutoa fursa kwa Sekta Binafsi na Asasi za Kiraia kuwasilisha hoja na masuala mbalimbali ambayo hufanyiwa maamuzi kupitia vikao rasmi. Pia, wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kupitia Mabunge ya nchi zao hufanya uchaguzi wa Wabunge wanaowawakilisha nchi hizo katika Bunge la Afrika Mashariki. Halikadhalika, Mahakama ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ina mamlaka ya kusikiliza mashauri mbalimbali kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa ukosoaji katika Jumuiya ya Afrika Mashariki unafanyika kupitia Bunge na Mahakama ya Afrika Mashariki. Bunge hilo limepewa mamlaka ya kusimamia utekelezaji wa shughuli za Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwa ni pamoja na kuandaa ripoti mbalimbali zinazowasilishwa na kujadiliwa ndani ya Bunge.

Hatua hii imewezesha Bunge hilo kutoa mapendekezo ya hatua za kuchukuliwa na Baraza la Mawaziri. Vilevile, kupitia Mahakama ya Afrika Mashariki wananchi hupeleka mashauri mbalimbali na Mahakama hiyo imeweza kufanya maamuzi ya kesi mbalimbali dhidi ya Serikali za nchi wanachama.