Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 5 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 58 2019-09-09

Name

Desderius John Mipata

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkasi Kusini

Primary Question

MHE. DESDERIUS J. MIPATA aliuliza:-

Wananchi wa Kijiji cha Kasapa walikuwa na ombi la kuongezewa maeneo ya kilimo kutoka kwenye eneo la Hifadhi ya Kalambo TFS:-

Je, Serikali imefikia hatua gani katika utekelezaji wa ombi hilo la wananchi wa Kijiji cha Kasapa?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Desderius John Mipata, Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Hifadhi ya Msitu wa Kalambo River ulihifadhiwa rasmi kwa kupitia tangazo la Serikali Na. 105 la mwaka 1957. Msitu huo upo katika Wilaya ya Kalambo na Nkasi Mkoani Rukwa na una jumla ya hekta 41,958.

Mheshimiwa Spika, hifadhi hii imekuwa na umuhimu wa kipekee kwa uhifadhi wa viumbe haia na vyenye umuhimu wa kipekee wakiwemo tembo. Aidha, hifadhi ina umuhimu mkubwa katika kutoa huduma za Kiikolojia kama maji. Maji haya ni muhimu kwa matumizi ya wananchi wa eneo hilo, pia kwa ajili ya maporomoko ya Kalambo ambayo ni pili kwa urefu mita 240 Barani Afrika baada ya yale ya Victoria yaliyoko Zimbabwe.

Mheshimiwa Spika, aidha, maporomiko ya Kalambo yana upekee kwa kuwa ni moja ya vivutio muhimu ambavyo vinaendelezwa kuchangia ukuaji wa uchumi kupitia Sekta katika Mikoa ya Rukwa na Katavi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 5 Julai, 2017 Waziri wa Maliasili na Utalii alitembelea Hifadhi ya Kalambo na baadaye Vijiji vya Kisapa ili kusikiliza maombi yao ya uhitaji wa ardhi. Katika Mkutano huo, Mheshimiwa Waziri aliagiza TFS kushirikiana na Halmashauri kufanya upimaji na tathmini ya maeneo yanayolimwa na kutoa taarifa ya mapendekezo ya hatua stahiki zitakazochukuliwa.

Mheshimiwa Spika, kufuatia maelekezo hayo, TFS kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ilifanya soroveya na kubaini kuwa maeneo mengi ya vijiji hivyo yamo ndani ya hifadhi ya misitu. Katika kushughulikia changamoto ya migogoro hiyo Mheshimiwa Rais aliunda Kamati ya Wizara nane kisekta kushughulikia migogoro baina ya wananchi na hifadhi. Mojawapo ya maeneo yanayofanyiwa kazi na Kamati hiyo ni pamoja na ombi la kuongezewa ardhi kwa wananchi wa Vijiji vya Kisapa na King’ombe. Taarifa ya Kamati imewasilishwa kwa Mheshimiwa Rais kwa ajili ya kupata maelekezo. Namwomba Mheshimiwa Mbunge avute subira wakati tunasubiri maelekezo ya Serikali.