Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 46 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 393 2016-06-20

Name

Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Primary Question

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI aliuliza:-
Wilaya ya Lushoto ni miongoni mwa Wilaya kubwa na Kongwe nchini ambapo ina takribani watu laki tatu lakini haina Mahakama ya Ardhi hivyo Wananchi hufuata huduma hiyo hadi Wilaya ya Korogwe licha ya kwamba majengo tunayo:-
Je, ni lini Serikali itaanzisha Mahakama hiyo katika Wilaya ya Lushoto ili kuwapunguzia adha wananchi wake wanaofuata huduma hiyo Wilayani Korogwe?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Shabani Shekilindi naomba Waheshimiwa Wabunge wafahamu kuwa, lengo la Serikali la kuunda Mabaraza ya Ardhi katika kila Wilaya ni kusogeza huduma za utatuzi wa migogoro ya ardhi karibu na wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua hilo, katika mwaka wa fedha 2015/2016, Serikali kupitia Wizara yangu kupitia Gazeti la Serikali Namba 545 ilitangaza kuanzisha jumla ya Mabaraza 47 ambayo yataundwa nchini likiwemo Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya ya Lushoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu na unyeti wa utatuzi wa migogoro ya ardhi katika Wilaya Kongwe ya Lushoto tarehe 6 Julai, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi alizindua rasmi Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya ya Lushoto. Kuanzia tarehe hiyo, Baraza limeshaanza kutoa huduma kwa wananchi wote wa Wilaya ya Lushoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee nitoe shukrani zangu za dhati kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto kwa kutupatia jengo kwa ajili ya uanzishwaji wa Baraza hilo. Vilevile nitoe wito kwa Wakurugenzi wote nchini kuharakisha kutoa majengo kwa ajili ya ofisi za Mabaraza ili huduma hii muhimu iweze isogezwe karibu na wananchi na kuweza kupunguza kama siyo kumaliza kabisa kero mbalimbali za migogoro ya ardhi nchini.